Habari za Kitaifa

Serikali ya Afrika Kusini yawatimua Wakenya waliokuwa wakifanya kazi nchini humo bila kibali

Na MASHIRIKA, WINNIE ONYANDO December 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI ya Afrika Kusini imewakamata raia saba wa Kenya wanaotuhumiwa kufanya kazi nchini humo kinyume na sheria na bila kuwa na nyaraka hitajika.

Wakenya hao ambao waliingia nchini humo kama watalii walikutwa wakifanya kazi ya kuwasajili wale ambao wanaomba hifadhi ya wakimbizi kupitia mpango wa serikali ya Amerika.

Kulingana na mamlaka za Afrika Kusini, Wakenya hao ambao hawakuwa na nyaraka zinazowaruhusu kufanya kazi nchini humo, waliajiriwa na shirika moja lisilo la serikali nchini Kenya ambalo lilipewa mkataba wa kuwasajili raia Wazungu wa Afrika Kusini wanaotaka kuomba uhifadhi ya nchini Amerika.

Kukamatwa kwa Wakenya hao Jumanne, Desemba 16, 2025 kulifuatia upelelezi na uvamizi katika kituo kimoja cha kushughulikia maombi ya wakimbizi na walikutwa wakiandaa nyaraka za visa ili waweze kusafiri Amerika.

Maafisa wa Afrika Kusini wamesema kuwa watu hao hawakukamatwa kwenye eneo la kidiplomasia kama walivyodai maafisa wa Amerika.

Mwezi Oktoba mwaka huu utawala wa Rais Trump ulitangaza mpango wa kutoa hifadhi za wakimbizi kwa raia Wazungu wa Afrika Kusini maarufu kama Afrikaner wapatao 7,500 katika mwaka huu wa kifedha.

Idadi hii ni chini ya ile iliyokuwa imepangiwa ya watu 100,000 chini ya utawala wa Rais Joe Biden.

Baada ya hapo kundi la takribani watu 50 walifanikiwa kuhamia Amerika chini ya mpango huo.

Na tangu wakati huo, vikundi vidogo vidogo vimekuwa vikiondoka Afrika Kusini chini ya mpango huo.

Uhusiano kati ya serikali za Amerika na Afrika Kusini umeendelea kuzorota tangu Rais Trump aliporudi madarakani akikosoa uongozi wa Pretoria kwa sera ambazo zinakandamiza raia hao Wazungu.

Mwezi Machi mwaka huu, Amerika ilimtimua balozi wa Afrika Kusini na pia kuongeza kodi ya asilimia 30 kwa bidhaa zinazotoka kwenye nchi hiyo.