Serikali yafeli makataa ya vitabu shuleni kwa masomo ya Gredi 10
SERIKALI imefeli kutimiza makataa yake ya Januari kuhusu kusambaza vitabu vya kiada katika shule kote nchini, ikimudu tu kusambaza sehemu ya vifaa vinavyohitajika kufikia sasa.
Waziri wa Elimu Julius Ogamba alisema kwamba kiwango cha usambazaji vitabu kimefikia asilimia 60 kufikia Jumapili, Februari 1.
“Tumefika asilimia 60,” akasema Waziri Ogamba.
Waziri alikiri kuwa wanafunzi zaidi ya 450,000 wangali hawajapata vitabu ambavyo ni nyenzo muhimu kwa masomo yao.
Awali aliashiria kwamba masomo yanaendelea kote nchini huku Wizara ikifanya hima kutimiza makataa ya Januari 31 ya kusambazia shule kikamilifu vifaa vyote vinavyohitajika.
Wakati huo, Bw Ogamba alifafanua kuwa malimbikizi ya deni la Sh11 bilioni zinazodaiwa na wachapishaji ndicho kiini cha kuchelewesha kusambaza vitabu vya kiada vya Gredi 10, akisema sehemu ya deni hilo la muda mrefu imelipwa.
Mvutano huo uliacha idadi kubwa ya wanafunzi 1.13 milioni wa Gredi 10 kukaa bure au kutegemea masomo kidijitali walipojiunga na mwaka wa kwanza wa Sekondari Pevu.
Hata hivyo, akizungumza jana alipowatembelea walimu waliolazwa hospitalini Nairobi kutokana na ajali iliyotokea Jumamosi jioni iliyowaua wawili na kuwajeruhi wengine kadhaa, alisema vitabu hivyo vitasambazwa vyote kikamilifu katika muda wa wiki moja.
“Kufikia Februari 10, vitabu vyote vitakuwa vimesambazwa,” alisema Bw Ogamba.
Kuhusu usajili, Bw Ogamba alisema serikali imeafikia asilimia 98 ya wanafunzi waliojiunga na Gredi 10.
Wengi walifungiwa nje kwa sababu mbalimbali ikiwemo kukosa karo na mahitaji mengine muhimu.
Alisema baada ya agizo la Rais William Ruto kwamba wanafunzi wote waliofanya KJSEA hata ikiwa hawana sare wala karo waende shuleni, kufikia jana shule zilikuwa zimewapokea wanafunzi zaidi ya 1.1 milioni.
“Amri hiyo ilipotolewa, tulikuwa na asilimia 92 ya usajili wote hivyo basi kulikuwa na asilimia nane iliyobaki. Kufikia Jumapili, tulikuwa tumefanikisha asilimia 98. Hiyo ni zaidi ya wanafunzi 1.1 milioni,” alisema waziri.
Wadau wa elimu hapo awali walielezea wasiwasi kuwa kuchelewesha vifaa vya masomo huenda kukazidisha ukosefu wa usawa kati ya shule zenye raslimali za kutosha na zilizopo maeneo yaliyotengwa.
Ajali nje ya Shule ya Msingi ya City, Nairobi
Kwa mujibu wa polisi, dereva wa matatu alipoteza mwelekeo wa gari la abiria 33 na kugonga kundi la watu waliokuwa wakisherehekea chaguzi za Muungano wa Walimu wa Sekondari (Kuppet) nje ya Shule ya Msingi ya City, Nairobi.
Wikendi, walimu na wanafunzi kadhaa waliathiriwa katika visa tofauti vya ajali barabarani.
Ajali ya Jumamosi jioni jijini Nairobi, ilisababisha vifo vya watu wawili na 26 wakajeruhiwa, huku ajali nyingine iliyotokea Nyeri Jumamosi asubuhi, ikiwaua wanafunzi wawili na kujeruhi wengine 27, kulingana na wizara.
Waziri aliwahimiza watumiaji wote wa barabara kumakinika “kwa sababu kupoteza maisha ni uchungu tunaojua sote.”