• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Serikali yasutwa kwa kunyima vyombo vya habari matangazo ya kibiashara

Serikali yasutwa kwa kunyima vyombo vya habari matangazo ya kibiashara

HASSAN WANZALA Na RICHARD MUNGUTI

MUUNGANO wa wadau sekta ya habari umelalamika ukidai hatua ya Katibu wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) Edward Kisiang’ani kupeana matangazo ya kibiashara ya serikali kwa Shirika la Habari Nchini (KBC) na The Star, inalenga kukandamizi uhuru wa vyombo vya habari.

Akihutubu katika hoteli ya Sarova mnamo Jumatano, Rais wa Chama cha Wahariri Nchini (KEG) Zubeidah Kananu alisema hatua ya serikali kupendelea baadhi ya vyombo vya habari inaumiza sekta hiyo ambayo inatoa fursa muhimu za kazi.

“Serikali ikitaka mbinu za kufufua KBC ije tutaipa mawaidha, lakini hatua yake ya kubagua vyombo vya habari si haki,” akasema Bi Kananu.

Februari 2024, Chama cha Mawakili Nchini (LSK) kiliwasilisha kesi kikiomba Mahakama Kuu ifutilie mbali agizo matangazo yote ya serikali yachapishwe katika gazeti la The Star linalomilikiwa na Radio Africa Group.

Katika kesi iliyoshtakiwa katika mahakama ya Milimani, LSK ilisema agizo la Prof Kisiang’ani kwamba matangazo yote ya Serikali, mashirika ya serikali, vyuo vikuu na mashirika huru yawe yakitangaza habari zao katika Gazeti la The Star inakiuka haki.

Prof Kisiang’ani alitoa agizo hilo mnamo Januari 23, 2024.

Katika barua aliyowaandikia makatibu wakuu na vinara wa asasi za serikali, Prof Kisiang’ani aliamuru matangazo yote yachapishwe na Convergence Media na Star Publications Limited.

“Agizo hili ni ukiukaji wa sheria na mwongozo wa serikali kwamba habari muhimu za serikali zipashwe umma na magazeti yanayosomwa kusambazwa kote nchini,” afisa mkuu wa LSK Bi Florence Muturi alidokeza katika kesi iliyowasilishwa katika mahakama ya Milimani.

LSK ilisema kwamba serikali huchapisha matangazo yake katika jarida la My-Gov kwa lengo la kuwapasha Wakenya wote habari muhimu, mwongozo wa serikali, kusaka utoaji wa huduma kwa umma, kusaka ajira kwa serikali na utoaji wa huduma nyingine muhimu za serikali.

Jarida hilo la Serikali lilikuwa likisambazwa na magazeti manne ya humu nchini ambayo ni Daily NationThe StandardThe Star, na The People Daily. Kandarasi ya kusambaza jarida hili la My-Gov iliisha Desemba 2023.

Baada ya kandarasi hii kukamilika muda wake, serikali iliweka matangazo kualika kampuni za magazeti kusambaza My-Gov.

Badala ya serikali kusubiri kampuni zenye uwezo kusambaza My-Gov kushiriki, iliteua The Star kinyume cha sheria, inasema LSK.

LSK inasema waziwazi kwamba The Star sio Gazeti linalosambazwa kote nchini bali lina soko kubwa jijini Nairobi.

Hii inamaanisha jarida la My-Gov  litatakuwa linasambazwa Nairobi tu.

Bi Muturi alisema Serikali haikufanya mashauri ya kutosha na washika dau ama kuwahoji Wakenya wanaopokea huduma zake kabla ya kuiteua The Star kusambaza My-Gov.

Wakili huyo alieleza mahakama kwamba Serikali haikushirikisha umma na kupata maoni ya umma kabla ya kuipa The Star kandarasi hiyo.

“Serikali ilichukua hatua hii kabla ya kufanya mahojiano na umma na washika dau kulingana na  Vifungu vya Katiba nambari 10(2) na 201,” akasema Bi Muturi katika kesi aliyowasilishwa kwa sheria za dharura.

Alisema serikali imekaidi sheria kupitia uteuzi wa The Star kusambaza My-Gov na kuomba mahakama kuu ifutilie mbali uamuzi huo.

“Kuteua The Star kusambaza My-Gov, serikali imepotoka na kukaidi sheria na uhuru wa vyombo vya utangazaji kielektroniki, magazeti na aina nyingine za usamabazaji habari. Sheria imepinga serikali kutamalaki usambazaji wa habari kupitia njia yoyote ile,” alisema Bi Muturi.

LSK ilisema kwamba serikali ilibagua kampuni nyingine ilipoteua The Star.

Pia LSK ilisema serikali ilikaidi kifungu nambari 35 (3) kinachosema usambazaji wa habari kwa umma utekelezwe na kampuni iliyo na uwezo wa kuwafikia watu wengi.

LSK ilisema Prof Kisiang’ani hana mamlaka kuwapa maagizo wakuu wengine wa mashirika na asasi za serikali.

  • Tags

You can share this post!

Korti yampa Nyashinski siku 14 kuwasilisha mkataba wa dili...

Mamake Jowie: Nina imani mwanangu ataachiliwa huru

T L