Habari za Kitaifa

Serikali yatupa Nemis ya Uhuru, yazindua Kemis kusajili wanafunzi Gredi ya 9

Na WINNIE ATIENO June 3rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WANAFUNZI wa Gredi ya Tisa watajiunga na shule za sekondari mwaka ujao kwa kutumia mfumo mpya wa kielektroniki wa kuwasajili wanafunzi maarufu kama KEMIS.

Serikali imebuni mfumo huo wa kieletroniki kuhakikisha wanafunzi wote walioko Gredi ya Tisa wanajiunga na shule za sekondari.  Katibu katika Wizara ya Elimu Prof Julius Bitok alitangaza kuwa wanafunzi milioni 1.2 walioko Gredi ya Tisa watajiunga na Gredi ya 10 katika shule za sekondari mwakani.

Mfumo huo wa kieletroniki uliovumbuliwa wiki iliyopita jijini Nairobi utanakili wanafunzi wote nchini kwanzia chekechea, shule za msingi, shule za upili, taasisi za kiufundi na vyuo vikuu.

“Tutatumia mfumo mpya wa KEMIS kuhakikisha wanafunzi wote walioko Gredi ya Tisa wanajiunga na Gredi ya 10 bila yeyote kuachwa nyuma. Tunatarajia wanafunzi 1.2 milioni wajiunge na shule za upili na kila kitu kiko tayari,” akasema Profesa Bitok.

Akiongea kwenye sherehe za kutuza wanafunzi bora katika shule ya upili ya Baringo, Prof Bitok alisema kila mtoto atapata nafasi katika shule za sekondari.

Hii ni licha ya kuwa na shule chache za sekondari nchini. Kulingana na takwimu katika wizara yake kuna shule 10,000 za sekondari na wazazi wameanza kueleza wasiwasi wao huku idadi ya wanafunzi ikiwa kubwa ikilinganishwa na shule za sekondari.

Wazazi wanahofu kuwa huenda kukawa na msongamano mkubwa katika shule za sekondari. Prof Bitok alisema Rais William Ruto amewekeza katika sekta ya elimu na kuhakikisha inapokea bajeti kubwa.

“Rais ameipa kipaumbele sekta ya elimu, anataka kuhakikisha kila mtoto anapata elimu bora ndio maana serikali yake imeweka kila mikakati ya kuhakikisha watoto wote wanajiunga na shule za sekondari bila changamoto zozote,” alisema Prof Bitok.

Awali wizara hiyo ilikuwa ikitumia mfumo wa NEMIS kuchukua takwimu ya wanafunzi katika shule za umma ndiposa itume mgao wa fedha za elimu ya bure. Hata hivyo, KEMIS sasa itachukua nafasi ya NEMIS.

“Mfumo huu utasaidia pakubwa kufuatilia maendeleo ya mtoto akiwa chekechea hadi pale atakapoachia ama kumalizia masomo yake,” akaongeza Profesa Bitok.

Haya yanajiri siku kadhaa baada ya Kamati ya Bunge inayosimamia Elimu ikiongozwa na mwenyekiti wake  Julius Melly kuunga mkono mfumo huo akiitaka wizara hiyo kuhakikisha inanakili wanafunzi wote kote nchini.

“Lazima mfumo huu wa kieletroniki ufanye kazi, awali washikadau katika sekta ya elimu walikuwa wanalalamika kuhusu NEMIS wakisema siyo wanafunzi wote walinakiliwa. Tunataka KEMIS ifanye kazi vizuri,“ akasema Bw Melly.

Kwa muda wa miaka mitatu sasa walimu wakuu wamekuwa wakilalamika kuhusu mfumo wa NEMIS ambao ulizuia wanafunzi wengi kukosa mgao wa fedha za elimu ya bure.

Ili unakiliwe kwenye NEMIS lazima uwe na cheti cha kuzaliwa, hata hivyo wanafunzi wengi hawana stakabadhi hiyo huku walimu wakuu wakiisihi serikali kunakili vidole badala ya cheti hicho.