Serikali za kaunti zashindwa kukusanya ushuru wa Sh143 bilioni
SERIKALI za kaunti zinadai malimbikizi ya jumla ya Sh143 bilioni katika mapato ambayo hazijalipwa, hali inayofichua mapengo makubwa katika mifumo ya ukusanyaji ushuru huku zikikabiliwa na changamoto ya kufadhili huduma muhimu na miradi ya maendeleo.
Kwa mujibu wa ripoti mpya ya Mdhibiti wa Bajeti Margaret Nyakang’o, kufikia Desemba 31, 2025, deni hilo lilijumuisha Sh101.54 bilioni kutoka mapato ya ndani ya kaunti, huku salio likihusiana na madeni kutoka Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), iliyokuwa Hazina ya Taifa ya Bima ya Afya (NHIF), pamoja na taasisi nyingine za umma.
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa kaunti nyingi zinakabiliwa na mzigo mkubwa wa kifedha unaochangiwa na ukusanyaji hafifu wa mapato, ucheleweshaji wa mgao kutoka serikali kuu na ongezeko la matumizi ya kawaida.
Hali hii inaathiri moja kwa moja utoaji wa huduma kwa wananchi na kudhoofisha mipango ya maendeleo ya muda mrefu.
Sehemu kubwa ya mapato ambayo hayajakusanywa inatokana na kodi za ardhi, kodi za nyumba na ada mbalimbali za kaunti, baadhi zikiwa zimedumu kwa zaidi ya miaka mitano hadi kumi bila kufuatiliwa kikamilifu.
Ukosefu wa hatua madhubuti za kisheria na kiutawala umechangia madeni haya kuendelea kuongezeka.
Wachambuzi wa masuala ya utawala wanasema kiasi hicho cha fedha kina uwezo wa kubadilisha sura ya maendeleo nchini, ikiwa kingekusanywa ipasavyo.
Kinaweza kufadhili ujenzi na ukarabati wa hospitali za ngazi ya nne na tano, kuboresha miundombinu ya barabara na kuanzisha miradi ya maji katika maeneo mengi.
Hata hivyo, kaunti nyingi hazijaweka mifumo thabiti ya ukusanyaji madeni, badala yake zikitegemea mgao kutoka serikali kuu ambao mara nyingi huchelewa.
Aidha, maamuzi ya kisiasa yamechangia kuzorota kwa nidhamu ya kifedha, hasa pale baadhi ya kaunti zinapotoa misamaha ya kodi ya ardhi na madeni ya nyumba, hususan kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Kaunti ya Nairobi inaongoza kwa kuwa na malimbikizo mengi zaidi ikidai Sh65.39 bilioni, sawa na karibu asilimia 45 ya jumla ya malimbikizi yote.
Hii inajumuisha Sh55.4 bilioni za kodi ya ardhi, pamoja na madeni ya kodi ya nyumba na ada za biashara. Kampuni ya Kenya Power pekee inadaiwa na kaunti Sh5.6 bilioni za ada ya njia za umeme.
Kaunti ya Mombasa inafuata kwa malimbikizi ya Sh14.51 bilioni, huku Nakuru ikidai Sh13.84 bilioni—kiasi kinachozidi mara nne mapato yake ya ndani kwa mwaka mmoja.
Hali hii inaibua wasiwasi kuhusu uendelevu wa kifedha wa kaunti hiyo, hasa ikizingatiwa kuwa mishahara pekee inakadiriwa kufikia Sh7 bilioni kwa mwaka.
Kaunti nyingine zinazodai madeni makubwa ni pamoja na Kiambu (Sh5.61 bilioni), Kakamega (Sh2.83 bilioni), Kisumu (Sh2.32 bilioni), Kitui na Kisii miongoni mwa zingine, hali inayoonyesha kuwa tatizo hili limeenea kote nchini.
Kwa upande mwingine, baadhi ya kaunti zimeonyesha dalili za udhibiti bora wa mapato. Kaunti ya Homa Bay iliripoti Sh23.27 milioni pekee, huku Murang’a ikiwa na malimbikizi ya Sh40 milioni, zikionyesha kuwa mifumo madhubuti ya ufuatiliaji inaweza kuleta matokeo chanya.
Kwa ujumla, zaidi ya robo tatu ya kaunti bado hazijafikia malengo yao ya ukusanyaji mapato ya ndani, licha ya kuwa na uwezo wa kukusanya hadi Sh260 bilioni kila mwaka kulingana na Tume ya Ugavi wa Mapato (CRA).
Katika mwaka wa kifedha wa 2024/2025, kaunti zilikusanya Sh67.3 bilioni dhidi ya lengo la Sh87.67 bilioni.
Bi Nyakang’o anapendekeza hatua za haraka kuchukuliwa, ikiwa ni pamoja na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji, kutumia teknolojia ya kidijitali kufuatilia mapato, na kuimarisha ushirikiano na taasisi kama SHA ili kurejesha madeni.
Bila mageuzi hayo, anaonya kuwa kaunti zitaendelea kukumbwa na matatizo ya kifedha yatakayodhoofisha utoaji wa huduma kwa wananchi.