Shakahola:Mackenzie alivyopotosha waumini hadi kufa njaa akitumia dini
MSHUKIWA wa mauaji ya halaiki ya Shakahola Paul Mackenzie alitumia maandiko matakatifu na njama ya kinadharia kufundisha wafuasi wake itikadi kali kuhusu ya siku za mwisho .
Mahakama ya Shanzu iliambiwa kuwa mafundisho haya yalichangia pakubwa mamia ya watu kuhamia msitu wa Shakahola na kuangamia kwa njaa huku wakiamini kuwa ndiyo njia pekee ya kumuona Yesu.
Mtaalamu wa Siakolojia Dkt Oscar Githua alieleza mahakama kuwa mhubiri huyo tata alitumia uwezo na ushawishi wake mkubwa katika elimu ya kidini kufundisha itikadi kali ya kidini.
“Msimamo mkali ulidhihirika kupitia mavazi yao, namna walivyoomba na muonekano wao wa kimwili,” Dkt Githua aliambia Hakimu Mwandamizi Mkuu Leah Juma.Kwa mujibu wa mtaalamu huyo, kulikuwa na viashiria vitano vikuu vilivyohusisha mienendo ya kundi hilo na msimamo mkali, itikadi kali na hata ugaidi.
Mojawapo ya viashiria hivyo ni kuamini katika “maadili ya kiroho” kama vile dhana kwamba dunia haina thamani tena na kwamba mwisho wa dunia ulikuwa karibu.
Dkt Githua alichambua mahubiri ya video, maandiko na machapisho ya Mackenzie na kubaini kuwa maudhui yaliyotangazwa humo yalikuwa yakiakisiwa katika mitazamo na tabia za wafuasi wake.
Alisema wafuasi hao walikuwa tayari kujitolea kwa kiwango cha juu, ikiwemo kukubali kifo, kwa imani ya kutafuta utakaso wa kiroho.Mackenzie aliwafundisha wafuasi wake tofauti kubwa kati ya ulimwengu wa kiroho na ule wa kimwili, akiwaelekeza katika mtazamo kuwa huduma kama elimu, afya na taasisi za serikali ni ovu.
“Huduma Namba, kwa mfano, ilionekana kama alama ya 666. Walikuwa na imani kuwa kutafuta huduma za serikali ni sawa na kujitia unajisi na hivyo kutostahili kukutana na Yesu,” alisema.
Katika tukio la kutisha zaidi, Dkt Githua alifichua kuwa baadhi ya akina mama waliwahusisha watoto wao katika mfungo wa hadi kufa wakiwa wameaminishwa kwamba hiyo ilikuwa njia ya kiroho ya kupata wokovu.
“Ni jambo lisilo la kawaida kabisa, lakini baadhi ya akina mama waliwaruhusu watoto wao kufa kwa njaa kwa sababu ya kiwango cha juu cha msimamo mkali waliokuwa nao,” alisema.
Kulingana na shahidi huyo, Mackenzie aliwahadaa wafuasi wake kwa matumaini ya utakaso wa kiroho kupitia ujumbe wa hofu kuhusu siku ya mwisho. Alijenga taswira ya kuogofya kuhusu Mpinga Kristo, akitumia maandiko ya Biblia na tafsiri za kupotosha.
Kulingana na shahidi huyo, video na vitabu alivyochambua vilionyesha kwa Mackenzie alidai kuwa serikali zote duniani ni sehemu ya mfumo wa kishetani na kwamba Huduma Namba ilikuwa alama ya Mpinga Kristo.
”Ujumbe katika stakabadhi hizo zilieneza dhana ya ‘mpangilio mpya wa dunia’ (New World Order) na kuwashawishi wafuasi wake wajitenge na serikali na taasisi zake,” aliongeza huku akihojiwa na wakili wa Mackenzie Lawrence Obonyo.Video alizotoa zilikuwa na majina kama “Mpinga Kristo,” “Babeli Iliyoporomoka,” “Katiba ni Mambo ya Shetani” na “Mwanadamu ni Shetani.”
Miongoni mwa vitabu vilivyochunguzwa na Dkt Githua ni ‘The New World Order’ kilichoandikwa na Mmarekani mwenye utata, ambacho kilijaa njama za kinadharia nyingi .
Dkt Githua alieleza mahakama kuwa maudhui yaliyokuwa katika mahubiri ya Mackenzie, vitabu na machapisho mengine yalikuwa na mlinganisho thabiti na matukio ya kihistoria ya madhehebu hatari duniani.
Alitaja tukio la mauaji ya Shakahola, ambapo zaidi ya watu 400 walifariki, kuwa sawa na vifo vya zaidi ya wafuasi 700 wa Movement for the Restoration of the Ten Commandments of God nchini Uganda mnamo mwaka 2000.Pia , aliilinganisha na tukio lilisababisha vifo vya watu 88 waliokufa katika makabiliano kati ya vikosi vya usalama na mhubiri David Koresh wa kundi la Branch Davidians huko Texas, Amerika.
Mahakama ilielezwa kuwa Kanisa la Mackenzie la Good News International na mauaji ya Shakahola yalifanana na kisa cha mwaka 1978 ambapo zaidi ya watu 900 wa dhehebu la People’s Temple waliuawa huko Jonestown, Guyana, chini ya uongozi wa Jim Jones.
“Shakahola ni kama chapa halisi ya matukio hayo matatu. Wafuasi walilazimishwa kujitenga na jamii, wakapelekwa maeneo ya porini ambapo hakukuwa na uangalizi wa serikali,” alisema Dkt Githua akiongozwa na viongozi wa mashtaka Jami Yamina, Victor Owiti and Betty Rubia.
Aliongeza kuwa katika matukio yote haya, viongozi wa dhehebu hizo tata walikuwa na mamlaka yasiyopingwa juu ya wafuasi wao , na mara nyingi walihusika katika ukatili na mateso ya kimwili na hata kihisia dhidi ya wafuasi wao.
“Matumizi ya mabavu, amri kali kutoka kwa viongozi na kutii bila kuuliza masuali ni mambo yaliyoshuhudiwa katika matukio yote haya. Mwisho wake huwa ni vifo vingi na mateso makubwa,” alihitimisha.Mackenzie pamoja na washirika wake 93 wanakabiliwa na mashtaka kadhaa ya jinai, yakiwemo ya kuchochea misimamo mikali na ushawishi wa kigaidi.