Aga Khan yauza hisa zake za Nation Media Group kwa Taarifa Limited ya Tanzania
SHIRIKA la maendeleo la Aga Khan (AKFED) limetangaza kuuza hisa zake zote za kampuni ya habari ya NMG kwa Taarifa Limited inayomilikiwa na Bw Rostam Azizi, mfanyabiashara Tanzania.
Bw Azizi ana biashara nyingi katika sekta mbali mbali ikiwemo habari, uchimbaji madini, kilimo, ujenzi miongoni mwa zingine.
Shirika hilo la Aga Khan lilisema kwenye taarifa Jumanne kwamba limeingia kwenye makubaliano ya kuuza hisa zake zote kwa Taarifa Limited. Aga Khan ilikuwa inamiliki asilimia 54.08 katika Nation Media, kwa maana hiyo ilikuwa mmiliki mwenye usemi mkubwa katika kuendesha biashara hiyo ya habari.
Kununuliwa huko kunamaanisha kwamba usimamizi wa Aga Khan katika kampuni hii ya habari ambao umedumu kwa miaka 66 sasa umetamatika, hivyo kuiweka Nation katika mikono ya Taarifa Limited.
Aga Khan ilianzisha Nation Media mnamo 1959.
“NMG sasa imejiweka pazuri kuimarisha uwezo wake kwa kuwekeza zaidi katika mabadiliko ya kidijitali. Taarifa Limited imejitolea kufanikisha mabadiliko haya na kusaidia shirika kuboresha uhusiano wake na wateja na kuendeleza tamaduni yake ya miaka mingi ya uanahabari unaoshughulikia maslahi ya mwananchi,” ikasema taarifa ya pamoja ya Akfed na Taarifa Limited.