Habari za Kitaifa

Sifuna aambia Oburu: Siendi popote, tukutane kortini

Na FATUMA BARIKI February 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SENETA wa Nairobi Edwin Sifuna ametaja kuvuliwa cheo cha Katibu Mkuu wa ODM kuwa ukiukaji mkubwa wa sheria na kwamba hatua hiyo haina mashiko na ataendelea kuhudumu kwenye wadhifa huo.

Akizungumza na wanahabari katika mkahawa wa Panafric, Nairobi akiwa ameandamana na Gavana James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Mbunge wa EALA aliye pia binti ya marehemu Raila Winnie Odinga pamoja na wabunge na madiwani wengine, Seneta Sifuna alishangaa iweje uamuzi kama huo uchukuliwe bila kufuata taratibu za Chama.

“Wamesema wamenitimua kwa kukosa nidhamu. Mbona sijawahi kuitwa na Kamati ya Nidhamu nielezewe makosa yangu na kupata fursa ya kujitetea?” akauliza.

Bw Sifuna alizungumza siku moja baada ya Baraza Kuu la ODM (NEC) likiongozwa na Kinara wa chama Oburu Oginga kukutana Mombasa ambapo walitangaza kumfurusha seneta huyo kutoka kwa uongozi wa chama.

Baraza hilo lilimteua Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Busia Catherine Omanyo kuwa Kaimu Katibu Mkuu huku likitangaza mkutano mkuu wa wajumbe (NDC) kufanyika Machi 27, 2026. Baraza hilo pia lilitangaza kuanza mchakato wa kujiondoa rasmi kutoka kwa Muungano wa Azimio la Umoja.

Seneta Sifuna alisema katiba ya chama haikufuatwa katika kumtimua na kwa sababu hiyo ataendelea kuhudumu kama Katibu Mkuu huku akipinga kufurushwa kwake kortini.

Kwa upande wa Gavana wa Siaya James Orengo,  alitilia mkazo kwamba Sifuna haendi kokote na kwamba ataendelea kuzungumza kwa niaba ya chama huku akimlaumu Rais William Ruto kwa kuingilia shughuli za ODM.

“Nashangaa kwamba limbukeni wanaweza kuongea kuhusu Sifuna. Sifuna anazungumza kwa niaba ya chama, hata sasa hivi na ataendelea na kazi. Rais Ruto, tafadhali achana na ODM,” akasema Bw Orengo.

Naye Babu Owino alisema ilikuwa ajabu kwamba katiba ya chama haikufuatwa, na kwamba waliokwenda Mombasa walishiriki mkutano haramu wa ‘Kangaroo court’ akisisitiza kwamba hatua yao imetangaza vita rasmi na kuwataka wajiandae kwa mapambano.

Mpasuko katika ODM umekuwa ukitokota tangu kufariki kwa mwanzilishi Raila Odinga Oktoba 15, 2025. Lakini kile kilichofasiriwa na wengi kuwa kutonesha kidonga kilikuwa mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika Busia wikendi iliyopita ambako mrengo wa Sifuna ulizindua kampeni ya Linda Mwananchi.

Kampeni hiyo ilichukuliwa kujibu ile inayoongozwa na Seneta Oginga ya Linda Ground ambayo imekuwa ikienda katika miji mbali mbali kukutana na wafuasi wa ODM.