Habari za Kitaifa

Sifuna akaa ngumu, afaulu kushawishi korti kuzima Msajili wa Vyama kutekeleza uamuzi wa ODM

Na BENSON MATHEKA, KEVIN CHERUIYOT February 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

SENETA wa Nairobi Edwin Sifuna amekataa katakata uamuzi wa Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) ya Chama cha Orange Democratic Movement (ODM) wa kumng’oa katika wadhifa wa Katibu Mkuu, akisisitiza kuwa bado ndiye kiongozi halali aliyechaguliwa kushikilia wadhifa huo.

Jana, mahakama inayotatua mizozo katika vyama vya kisiasa ilizima kutimuliwa kwake kama Katibu Mkuu wa ODM na ikazuia kuchapisha kuondolewa kwake na msajili wa vyama vya kisiasa hadi kesi aliyosilisha itakapoamuliwa.

Katika agizo lake, mahakama hiyo ilisitisha utekelezaji wa maazimio ya kikao cha NEC ya ODM kilichofanyika Mombasa ambapo tangazo la kumvua Sifuna wadhifa wake lilitangazwa.

Katika kesi hiyo, Sifuna ameshtaki ODM na Msajili wa vyama vya kisiasa. jijini Nairobi kabla ya uamuzi wa korti, Sifuna alisema hatua iliyochukuliwa na kikao cha NEC kilichofanyika Mombasa Jumatano ni kinyume cha katiba ya chama na inakiuka haki zake za kimsingi kama mwanachama wa ODM.

“Nimepokea tangazo lililotolewa na sehemu ya NEC kule Mombasa wakidai kuniondoa katika wadhifa wa Katibu Mkuu. Nataka kusema bila woga wowote kwamba, hatua hiyo ni kinyume cha sheria, haikufuata taratibu na ni uvunjaji wa wazi wa Katiba ya ODM pamoja na kanuni za haki asilia,” alisema Sifuna.

Aliongeza: “Ninasalia kuwa mwanachama mwaminifu na Katibu Mkuu halali aliyechaguliwa wa ODM. Nitaendelea kujitolea katika mapambano ya Kenya yenye haki, usawa na demokrasia.”

SOMA PIA: Sifuna atangaza mkutano mkubwa wa hadhara saa chache baada ya kutemwa na ODM

Uamuzi wa kumwondoa Sifuna ulitangazwa Jumatano baada ya kikao cha NEC Mombasa. Katika taarifa, chama kilisema baada ya kujadili mwenendo wa Sifuna, kiliazimia kumvua majukumu yake mara moja na kumteua Naibu Katibu Mkuu Catherine Omanyo kushikilia wadhifa huo kwa muda.

Hata hivyo, Sifuna amedai kuwa hakuwahi kupewa notisi ya tuhuma zozote wala kuitwa kujitetea.

“Hakuna wakati wowote nilijulishwa madai yoyote dhidi yangu, iwe ni utovu wa nidhamu au uzembe. Wala sijawahi kuitwa kujibu malalamishi yoyote,” alisema.

Seneta huyo alihusisha kuondolewa kwake na msimamo wake mkali wa kupinga mipango ya kumuunga mkono Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027.

“Kosa langu pekee ni kukataa na kupinga mpango wowote ndani ya chama wa kumuunga mkono Rais Ruto kwa muhula mwingine. Nimekuwa, na nitaendelea kuwa na msimamo kwamba nchi hii haiwezi kumudu miaka mingine mitano ya uongozi huu ghali na usio na mwelekeo,” alisema.

Aidha, Sifuna alikosoa mabadiliko ya hivi karibuni ya uongozi ndani ya ODM, akidai uteuzi wa Dkt Oburu Odinga haukufuata taratibu za katiba ya chama.

Alisema hatua za haraka na zisizo za kikatiba zinaashiria kupuuza misingi ya taasisi za kidemokrasia.

Katika mkutano huo na wanahabari, Sifuna aliandamana na viongozi kadhaa mashuhuri wa ODM wakiwemo Naibu Kiongozi wa Chama Godfrey Osotsi, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na Mwanachama wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) Winnie Odinga.

Wote walisisitiza kuwa Sifuna bado ni Katibu Mkuu halali. Mbunge Babu Owino alitaja kikao cha NEC kilichomng’oa Sifuna kuwa haramu, akisema hakikuwa kimeundwa kisheria.

“Haiwezekani viongozi walioko madarakani kinyume cha sheria wamwondoe kiongozi aliyechaguliwa kihalali. Kosa pekee la Sifuna ni kupigania wanyonge, ajira kwa vijana na kupinga gharama ya juu ya maisha,” alisema Babu.

SOMA PIA: Sifuna aambia Oburu: Siendi popote, tukutane kortini

Bw Sifuna alitangaza kuwa ataendelea na mikutano ya “Linda Mwananchi” kote nchini, akisema sauti ya wanachama haiwezi kunyamazishwa.

Alisema mkutano wa kwanza baada ya kuondolewa kwake utafanyika Kitengela, Kaunti ya Kajiado, Jumapili ijayo kabla ya kuelekea Vihiga, Kakamega, Bungoma na Kisii.

Seneta huyo alisema atatumia mbinu zote kulinda wadhifa wake ikiwemo kwenda kortini.

Kuondolewa kwa Sifuna kunajiri katika kipindi cha misukosuko ndani ya ODM kufuatia kifo cha aliyekuwa kiongozi wa chama, Raila Odinga mwaka jana.

Mgawanyiko wa wazi sasa umeibuka kati ya makundi  yanayopingana kuhusu mwelekeo wa chama na ushirikiano wake na serikali ya UDA.

Wachambuzi wa siasa wanasema mvutano huo unaweza kuathiri mustakabali wa ODM kuelekea Mkutano wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) uliopangwa kufanyika Machi 26, ambapo wajumbe watapata fursa ya kuchagua maafisa wa chama.

Bw Sifuna na kundi lake la Linda Mwananchi walitangaza kuwa watahudhuria mkutano huo wa wajumbe wakisema wangali wanachama na viongozi waliochaguliwa kwa tiketi ya ODM.

UNAWEZA KUPENDA: Otiende naye pia aanza kuongea lugha ya Sifuna