Habari za Kitaifa

Sifuna akabiliwa na maamuzi magumu akifika mbele ya Kamati ya Nidhamu ya ODM

Na MOSES NYAMORI April 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KATIBU Mkuu wa ODM Edwin Sifuna anakabiliwa na mtihani mgumu ambao utamjenga au kumponza kisiasa wiki hii akitarajiwa kufika mbele ya Kamati ya Nidhamu ya chama hicho kujibu maswali kuhusu mienendo yake.

ODM imempa Seneta Sifuna hadi Aprili 8 kujibu barua aliyoandikiwa yenye maswali kuhusu mienendo yake kisha afike kujitetea mbele ya kamati hiyo mnamo Aprili 10.

Bw Sifuna ana maamuzi matatu muhimu ya kufanya; au abakie katika chama cha ODM na aendelee kupambana na utawala wa Rais William Ruto hadi mwisho, aunde chama kipya cha kisiasa, au aungane na Muungano wa Upinzani.

Wachanganuzi wa kisiasa tayari wanasema itakuwa vigumu kwa Bw Sifuna kuponea mara hii baada ya Jopo la Kutatua Mizozo ya Kisiasa (PPDT) kumnusuru kwa kuamua kuwa ODM haikutumia njia zote kusuluhisha mgogoro naye kabla ya kumtimua.

Hata akisalia ODM, bado Bw Sifuna atakabiliwa na masaibu zaidi kwa kuwa chama hicho tayari kimeanza kujipanga bila yeye.

Hata kupata tiketi ya kuwania itakuwa vigumu baada ya mbunge wa Lang’ata Phelix Odiwuor maarufu kama Jalang’o kutangaza atagombea useneta wa Nairobi kupitia ODM.

Aidha, Kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga katika Kongamano la Wajumbe (NDC) mwezi uliopita alitangaza kuwa sasa hatawavumilia wanaompinga chamani akiapa kupambana nao kuhakikisha kuna nidhamu ndani ya ODM.

Mbunge wa Nyeri Mjini, Ngunjiri Wambugu anasema Bw Sifuna atanufaika tu kisiasa akisalia ODM.

“Namshauri apiganie nafasi yake ndani ya chama kwa sababu hata asipopata kila kitu, atafanikiwa kupata kitu. Hakuna mtu ambaye amewahi kung’aa kisiasa kama mtu binafsi, na leo Sifuna ana umuhimu kwa sababu ya ODM,” akasema Wambugu.

Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi ambaye alifurushwa kama naibu kiongozi wa ODM anasema Bw Sifuna hana nafasi ya kuokoa wadhifa wake.

“Viongozi wa ODM wanamfanyia kazi Rais Ruto ambaye lazima ataridhishwa na uamuzi wa ODM. Wamemsaliti Raila kwa mamlaka feki na pesa,” akasema Osotsi.

Mchanganuzi wa siasa, Rachel Omollo naye anasema, “Anastahili kujisawiri kama anayedhulumiwa na ODM na ataendelea kuwa maarufu,” akasema Bi Omollo.

Kuhusu kujiunga na upinzani, mchanganuzi wa siasa Javas Bigambo anasema, “Bw Sifuna alijizolea umaarufu kwa sababu ya Raila na huo umaarufu hauwezi kuhamishwa kwa upinzani. Wale ambao walikuwa waaminifu kwa Raila wataanza kumwangalia kwa jicho la usaliti kwa sababu baadhi ya viongozi wa upinzani walikuwa maadui wa Raila.”

Naye Prof Macharia Munene anasema ni kupitia Bw Sifuna kuungana na upinzani ndipo kutasaidia kuhakikisha Rais Ruto anahudumu kwa muhula mmoja.

Katika mojawapo ya mahojiano na vyombo vya habari, Bw Sifuna alionyesha utayarifu wa vuguvugu la Linda Mwananchi kushirikiana na Upinzani unaoongozwa na kiongozi wa DCP, Rigathi Gachagua pamoja na Kalonzo Musyoka katika kumwondoa Dkt Ruto madarakani.

“Ningependa kuwahakikishia wote wanaoamini kwamba nchi yetu haiwezi kustahimili muhula mwingine wa Ruto, kuwa hatutakuwa kikwazo. Sisi sote lazima tukubaliana na kusema huu ndio mpango utakaompeleka huyu jamaa nyumbani,” aliambia kipindi cha Fixing the Nation cha NTV majuzi.

Naibu Gavana wa Kakamega, Ayub Savula anasema iwapo Sifuna ataamua kujijenga kupitia vuguvugu lake la Linda Mwananchi basi siasa zake zimeisha.

“Baadhi ya Gen-Z anaodai anao hata hawajisajili kupiga kura na wengine hawako Nairobi kumsaidia ahifadhi kiti chake. Anastahili kuamua kufanya kazi na Dkt Oburu ili ajiimarishe zaidi kisiasa.”

Mhadhiri Prof David Monda anayefundisha Amerika anasema nafuu pekee kwa Bw Sifuna akiamua kujisimamia kisiasa ni awanie urais 2027.

“Anaweza kuwania urais lakini hii pia itanufaisha Rais Ruto kwa kulemaza makali ya upinzani,” akasema Prof Monda.

Seneta Sifuna na mrengo wake wa Linda Mwananchi wanaendelea kupata nguvu kwa kupinga utawala wa Rais Ruto.

Ndani ya ODM, wanaopinga Serikali Jumuishi na kambi ya Linda Ground ya Dkt Oburu, wamejinasibisha na Linda Mwananchi.

Hali hiyo imezua tetesi kwamba Bw Sifuna na kikosi chake kinachoasi ODM, wakiwemo Seneta Osotsi, Gavana wa Siaya James Orengo, wabunge Babu Owino (Embakasi Mashariki), Anthony Kibagendi (Kitutu Chache Kusini), Caroli Omondi (Suba Kusini) na Wilberforce Ounda (Funyula), wanaweza kufikiria kuunda chama kipya cha kisiasa.

Msukosuko wa hivi karibuni kuhusu jaribio la kuhifadhi jina la chama kwa Msajili wa Vyama uliongeza uzito katika tetesi hizo.