Siku 1000 za Ruto: Ukatili wazidi chini ya uongozi wa Kenya Kwanza
RAIS William Ruto anapotimiza siku 1,000 madarakani, Kenya inaning’inia kwenye ukingo hatari.
Matumizi ya nguvu kupita kiasi wakati wa maandamano, vitisho dhidi ya uhuru wa kujieleza, kuungana na kukusanyika, kufurushwa, kukamatwa na kuzuiliwa kiholela pamoja na watu kupotezwa ni baadhi ya ukiukaji wa haki za binadamu unaohusishwa na utawala wake wa miaka miwili na nusu.
Tangu 2022 mwaka ambao Rais Ruto alichukua madaraka, takriban Wakenya 352 wameuawa kupitia mauaji ya kiholela.
Haya ni kwa mujibu wa ripoti ya hivi karibuni kutoka kwa Missing Voices Coalition, muungano wa mashirika kadhaa ya kijamii, ambayo ilitoa takwimu kuhusu matukio ya kutoweka na mauaji nchini tangu 2022.
Ni muhimu kutambua kuwa mwaka 2022, ambao unachangia vifo 130 kati ya hivyo, ulikuwa chini ya uongozi wa Rais wa zamani Uhuru Kenyatta, ambaye aliondoka madarakani Agosti, akimwachia mamlaka Dkt Ruto ambaye alikuwa Naibu wake.
Mnamo mwaka 2023, Wakenya 118 walifariki mikononi mwa maafisa wa usalama wa serikali, na idadi hiyo ikapungua kidogo hadi 104 mwaka 2024.
Kuhusu watu kupotezwa kwa lazima, watu 87 wametoweka kabisa.
Idadi kubwa ya watu hao 55 walitoweka mwaka 2024, hasa wakati na baada ya maandamano dhidi ya Mswada wa Fedha wa 2024.
Kile kilichoanza kama ahadi za mageuzi ya kikatiba na haki za binadamu kutoka kwa Rais Ruto kimegeuka kuwa kipindi cha giza cha ukatili wa serikali, utekaji nyara, na serikali inayotuhumiwa kuongoza kwa kuzua hofu.
Utawala wa Kenya Kwanza, ambao awali ulionekana kama nuru baada ya ukandamizaji chini ya serikali ya Jubilee, sasa unakabiliwa na tuhuma kali za kufufua mbinu zile zile walizopinga: kutoweka kwa lazima, mauaji ya kiholela, na ukwepaji wa sheria unaohalalishwa na taasisi za serikali.
Kati ya Juni na Desemba 2024, angalau Wakenya 82, wengi wao wakiwa vijana, waliotoa sauti zao mitandaoni, walitekwa nyara kutoka majumbani mwao, mitaani na hata wakisafiri kwa magari ya umma, kulingana na takwimu za Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu ya Kenya.
Kosa lao, kulingana na mashirika ya haki za binadamu, lilikuwa ni kukosoa serikali.
Mashirika ya Human Rights Watch na Amnesty International, yameripoti simulizi za kutisha: vijana waliofungwa macho na kutupwa misituni, kuteswa kwa siku kadhaa, kuhojiwa kuhusu mipango ya maandamano, na kuonywa “nyamazeni au mtatoweka kabisa.”
Wengi wao hawajawahi kuonekana tena. Wazazi wamewasilisha ripoti kwa polisi, kuajiri mawakili, na kuwatafuta wanao katika mochari, bila mafanikio.
Kile kilichoanza kama uasi wa kiraia kiligeuka kuwa mauaji yaliyoidhinishwa na serikali, huku polisi wakishtumiwa kwa kufyatulia risasi waandamanaji.
Moshi wa vitoa machozi uliwadhuru hata watoto darasani.
Kwa mujibu wa Mamlaka Huru ya Usimamizi wa Polisi (IPOA), watu wasiopungua 67 walifariki dunia.
Mwishoni mwa Aprili 2025, siku chache baada ya BBC kupeperusha uchunguzi uliofichua maafisa wa usalama waliowapiga risasi waandamanaji mbele ya Bunge Juni 25 2024, IPOA ilitangaza kuwa ilikuwa imemaliza uchunguzi 22, ikiendelea na nyingine 36, na kuwa maafisa wawili tayari wameshtakiwa mahakamani.
Miongoni mwa waathiriwa wa maandamano ya kizazi cha Gen-Z alikuwa Denzel Omondi, mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo na Teknolojia cha Jomo Kenyatta mwenye umri wa miaka 21, ambaye hakurudi nyumbani baada ya maandamano.
Mwili wake uliokuwa na majeraha ulipatikana baadaye kwenye kidimbwi cha maji.
Polisi walidai kuwa uchunguzi unaendelea, lakini kama kesi nyingi nyingine, hakuna yeyote aliyewajibishwa.
Akihutubia taifa katikati ya maandamano dhidi ya Mswada wa Fedha wa 2024, Naibu Rais Kithure Kindiki, ambaye wakati huo alikuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, alisifu “uweledi” wa polisi wakati wa maandamano hayo.
Kwa familia za waathiriwa, ilikuwa kama dharau. Hali ilikuwa hivyo kwao wakati Rais Ruto, kwenye mahojiano ya moja kwa moja na runinga za kitaifa, alipozungumzia kifo cha Kennedy Onyango, mtoto wa miaka 12 aliyeuawa kwa risasi na polisi huko Rongai wakati wa maandamano ya Juni, kwa kuuliza, “bado yuko hai, sivyo?”
Jocinter Anyango, mama yake marehemu Kennedy, alitoa maneno ya uchungu kuhusu kauli ya Rais kwa kifo cha mwanawe.
“Hapo walinikosea sana. Niliendelea kumwomba Mungu, kwa nini mimi, kwa nini mwanangu? Kama angekuwa mtoto wa mtu tajiri, labda angepata haki. Sasa nimebaki na Mungu wangu,” aliambia Taifa Leo katika mahojiano Mei 20, 2025, takribani mwaka mmoja baada ya kifo cha mwanawe.