Trump: Tunajua anakojificha Ayatollah Khamenei na tunampa muda ajisalimishe
RAIS wa Amerika, Donald Trump sasa anasema kuwa Washington inafahamu alikojificha kiongozi wa Kidini wa Iran Ayatollah Ali Khamenei ambaye analengwa na Israeli huku vita vikiendelea kwa siku ya saba leo kila upande ukirusha makombora.
Kulingana na rais huyo, japo wanafahamu aliko kiongozi huyo wa kidini, hawana haja ya kumuua kwa sasa kwani wanataka ajisalimishe.
Katika ujumbe wake aliouchapisha kupitia mitandao ya kijamii, Trump aliitaka Iran “kusalimu amri bila masharti” huku mzozo huo ukizidi kuongezeka.
“Tunajua haswa anakojificha huyo wanayemrejelea kama ‘Kiongozi Mkuu.’ Ni rahisi kumpata lakini yuko salama huko aliko, hatutomuua angalau kwa sasa,” Trump alisema.
Ayatollah ambaye ana usemi kuhusu masuala yote ya uongozi wa Iran amekuwa na msimamo mkali huku akipinga vikali matakwa ya Amerika kwenye mazungumzo ya kutaka Iran ikome kukuza kiwanda chake cha nuklia na kutengeneza silaha hatari.
Matamshi hayo ya Trump yanajiri baada ya kuwahimiza wakazi zaidi ya milioni 9 wa Tehran kuondoka ili kuokoa maisha yao huku akikatiza ushiriki wake katika mkutano wa kilele wa nchi saba tajiri kiviwanda za G7 na kurejea Washington kwa mazungumzo ya haraka na washauri wake wa kiusalama.
Hapo awali, Trump alichapisha ujumbe mwingine akitangaza juu ya udhibiti kamili wa anga ya Tehran.
Iran kwa mara nyingine imefyatua makombora kuelekea Israeli huku nchi hiyo nayo ikiushambulia mji mkuu Tehran na miji mingine ya Iran. Hadi kufikia sasa, watu waliouawa nchini Israeli ni 24 na zaidi ya 600 kujeruhiwa. Na huko nchini Iran watu zaidi ya 200 wameuawa.
Wakati huo huo jeshi la ulinzi la Israeli IDF limeripoti mapema asubuhi ya Jumatano kwamba makombora zaidi kutoka Iran yanazidi kufyatuliwa.
Tahadhari ilitolewa huku jeshi la Israeli likiwahimiza raia wake kufuata maelekezo yanayotolewa na idara ya tahadhari ya IDF.
Netanyahu alisema watasambaratisha viongozi wa usalama wa Iran.
Ripoti hiyo inafuatia onyo lililotolewa na mkuu wa utumishi wa jeshi la Iran, aliyewataka watu kuondoka katika miji mikubwa ya Israeli ya Tel Aviv na Haifa.
Wakazi wa mji mkuu wa Iran walionekana pia wakiondoka mjini huku maduka na masoko ya kihistoria mjini Tehran yakifungwa Jumanne.
Rais wa China Xi Jinping ameelezea ‘wasiwasi wake mkubwa’ kuhusu kuongezeka kwa mvutano kati ya Israel na Iran na kusema kwamba serikali ya Beijing iko tayari kuingilia kati ili amani na utulivu upatikana katika eneo hilo.