Habari za Kitaifa

Tukio adimu Ramadhani na Kwaresma zikianza pamoja kesho

Na ANTONY KITIMO February 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HAPO kesho Waislamu na Wakristo kote duniani wataanza msimu wa kufunga, kuwazia uhusiano wao na Mwenyezi na safari ya kutakasa nafsi zao.

Kwa Wakatoliki watakuwa wakiadhimisha Jumatano ya majivu, inayoashiria mwanzo wa mfungo Kwaresma. Mfungo huo utadumu kwa siku 40 na siku za Ijumaa hawatajuwa wakila nyama.

Katika kipindi hiki Wakatoliki wanahimizwa kuepuka anasa za aina mbalimbali na kutojaamiana mkesha wa kila Jumapili.

Aidha katika kipindi chote cha Kwaresma, Wakatoliki wanahimizwa pia kujinyima angalau mlo moja na aina nyinginezo za anasa. Pesa watakazo okoa zitatumika kuwafaa maskini siku ya Pasaka.

Mbali na kufunga, kula, kunywa na anasa, Wakatoliki wanashauriwa kuzidishwa sala.

Waislamu nao wataanza Mwezi Mtukufu wa Ramadhan kesho iwapo mwezi utakuwa umeandama leo.

Ramadhan ni mwezi ambapo Mtume Mohamed (SAW) alishushiwa Quran na Waislamu hufunga kutoka asubuhi jua linapochomoza hadi jioni jua linapotua.

Ramadhan inatarajiwa kuwepo kuanzia Februari 18 hadi Machi 19 huku Kwaresma nayo ikikamilika Aprili 5 na kupisha Pasaka.

Mara ya mwisho ambapo Kwaresma na Ramadhan zilikuwa katika mwezi moja ni mapema miaka 90 na hii inatarajiwa kutokea miaka ya 2050s.

“Ramadhan huwa inazunguka kila mwaka hadi miaka 33 na huwa siku 11 mapema kila mwaka. Mara ya mwisho Ramadhan na Kwaresma zilikuwa mwezi moja ni mapema 90 na sasa imetokea tena,” ikasema jarida la Kisayansi la Astronomical Applications, Amerika.

Msomi wa Kiislamu Mohamed Khalifa alisema Kwaresma na Ramadhan kuwa mwezi moja mwaka huu kunatukumbusha kuhusu ubinadamu, amani, huruma na maelewano.

“Ramadhan inaeneziwa sana na Waislamu na ni kati ya nguzo tano za dini hiyo. Waislamu wote hufunga isipokuwa wale ambao ni wazee, wadogo kabisa, wajawazito na wanaosafiri,” akasema Sheikh Khalifa.

“Wanatarajiwa kujiepusha na mahaba na kutofanya maovu yoyote kuanzia kuchomoza kwa jua hadi kutua kwa jua,” akaongeza.

Kwenye miji ambayo kuna Waislamu na Wakristo, biashara zinatarajiwa zitapungua hasa hotelini. Baadhi ya wamiliki wa hoteli tayari wameanza kusaka njia nyingine ya kusaka riziki.

“Itabidi nifunge mwezi moja kufanyia hoteli yangu ukarabati kwa sababu hakutakuwa na biashara,” akasema Albert Mwaghesha, mmiliki wa hoteli Tudor, Mombasa.