Habari za Kitaifa

Tumieni mitandao ya kijamii kuanika wafisadi nchini, asema Mkuu wa Utumishi wa Umma

Na STANLEY NGOTHO December 10th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MKUU wa Utumishi wa Umma, Bw Felix Koskei, ametoa wito kwa Wakenya kushirikiana na serikali katika vita dhidi ya ufisadi ambao kwa miaka mingi umeathiri utoaji wa huduma za serikali.

Bw Koskei amesema kwamba licha ya hatua nyingi ambazo serikali ya Rais William Ruto imeweka kukabili janga hilo, ufisadi bado umeenea katika ngazi za mashinani kote nchini.

Amesisitiza Wakenya wana uwezo mkubwa kupitia mitandao ya kijamii kurekodi na kufichua maafisa wala rushwa kwa kutumia simu zao.

“Serikali imejizatiti kung’oa ufisadi ili kuboresha huduma kwa umma. Serikali kupitia taasisi husika iko tayari kumshtaki kila mfisadi, lakini Wakenya lazima wasimame na kutumia nguvu ya mitandao ya kijamii kuwafichua wanaoendeleza ufisadi,” alisema Bw Koskei.

Alisema hayo Jumanne katika Chuo Kikuu cha Cooperative wakati wa uzinduzi wa warsha ya Kamati za Uangalizi wa Wananchi Dhidi ya Ufisadi za Kaunti (CACCOCs), zinazolenga kujumuisha wananchi katika vita dhidi ya ufisadi.