Uchungu wagubika kijiji Kisii baada ya kijana Clinton Nyapara kufia vitani Ukraine
SIMANZI imegubika kijiji chenye utulivu cha Riateri, Bonchari, Kaunti ya Kisii, kufuatia kifo cha Clinton Nyapara Mogesa, 29, nchini Urusi, msiba ambao umeacha familia yake ikitafuta majibu.
Habari za kifo cha Bw Nyapara zimeachia wapendwa wake mshtuko, wakimwomboleza mwana wao aliyeondoka nyumbani kusaka riziki lakini akarejea akiwa ndani ya jeneza.
Akiwa mwingi wa matumaini kuhusu siku bora zijazo, Nyapara aliondoka kijijini chao 2024.
Sawia na vijana wengi Wakenya, alisafiri Doha, Qatar, akipania kuboresha maisha ya familia yake kabla ya hatima yake kuchukua mkondo tofauti ambao haukutarajiwa.
Kulingana na ripoti kutoka Taasisi ya Ujasusi Ukraine iliyotwikwa jukumu la kulinda taifa la Ukraine, mwili wa Nyapara uligunduliwa katika eneo lililotwaliwa na vikosi vya Urusi.
“Taasisi ya Ujasusi Ukraine ilitambulisha mwili wa Clinton Nyapara Mogesa, raia wa Jamhuri ya Kenya aliyezaliwa 1997,” ilieleza ripoti.
Ripoti hiyo vilevile ilifichua kuwa Nyapara aliishi na kufanya kazi Qatar kabla ya kutia saini mkataba na jeshi la Urusi ambapo alitumwa katika kituo chao kimoja.
Baada ya kupokea mafunzo kwa muda mfupi, aliuawa katika kilichoelezwa kuwa “shambulizi la kinyama” katika eneo la Donetsk.
Vikosi vya Urusi havikuondoa mwili wake. Alipatikana na pasipoti za Wakenya wengine wawili wanaoaminika kusajiliwa kwa njia sawia.
Nyumbani Kisii, uchungu wa kumpoteza uligubikwa na mshtuko na kuchanganyikiwa.
Bw Joel Mogere, kaka yake Nyapara alisema familia ilijitolea mhanga kufanikisha safari yake ng’ambo.
“Tuliuza sehemu ya ardhi ya familia kuwezesha kaka yangu kusafiri Qatar ili atusaidie baadaye. Hatukufahamishwa kwamba alisafiri Urusi na kusajiliwa kuwa mwanajeshi. Ndiye kitindamimba wetu na tegemeo. kuu Kifo chake kimetushtusha mno. Tulimtuma Qatar, na kusikia baadaye aliishia Urusi,” alisema Bw Mogere.
Mama yao, Mellen Moraa, alisema mwana wao alikuwa tegemeo lake kubwa hasa kwa mahitaji ya matibabu.
“Alikuwa anatusaidia na kila kitu. Nasihi serikali itusaidie,” alisema.
Familia ilifichua kwamba haimfahamu ajenti aliyewezesha mwana wao kusafiri ulaya.
Wamesihi Wizara ya Masuala ya Kigeni kuingilia kati kufuatilia haki ya mtoto wao, na kuwakamata watu wanaowahadaa vijana kwenda vitani kwa kisingizio cha ajira.
Aidha, wameirai serikali kuwasaidia kurejesha mwili wa jamaa wao kwa mazishi ya heshima nyumbani.
Kifo cha Nyapara kimejiri huku ripoti zikizidi kuongezeka kuhusu Waafrika, ikiwemo Wakenya, wanaosajiliwa kushiriki vita vya Urusi na Ukraine.
Mnamo Januari 31, 2026 Taasisi ya Ujasusi kuhusu Jeshi Ukraine ilionya raia wa kigeni dhidi ya kusafiri au kukubali kufanya kazi Urusi.