Habari za Kitaifa

Uganda debeni leo huku taharuki ikitanda baada ya serikali kuzima intaneti

January 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KAMPALA, UGANDA

WAPIGAKURA milioni 21.6 leo wanaelekea debeni nchini Uganda huku taharuki ikitanda baada ya serikali kutangaza kuwa itazima intaneti nao upinzani ukisema lazima kuwe na uchaguzi huru, wazi na wa haki.

Vituo vya upigaji kura vitafunguliwa saa 12 asubuhi kisha upigaji kura utamatike saa 11 jioni. Kando na uchaguzi wa urais, pia wapigakura watawachagua wabunge wapya.

Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Uganda Simon Byabakama alisema matokeo yanatarajiwa kutangazwa ndani ya saa 48 baada ya upigaji kura kumalizika. Hii ina maana mshindi lazima atangawe kabla Jumamosi saa 12 jioni.

Mnamo Jumatatu, Byabakama aliwaambia wanahabari kuwa, matokeo yatatangazwa kiwango cha wilaya kisha yatumwe kwa kituo kikuu cha kujumuisha kura Lubowa, Wilaya ya Wakiso.

Ndani ya siku hizo mbili tume itatathmini na kujumuisha kura kabla ya mshindi wa urais kutangazwa.

Rais Yoweri Museveni ametangaza Januari 15 na Januari 16 kama sikukuu ili kuwaruhusu Waganda kushiriki uchaguzi mkuu.

Farasi ni wawili kwenye uchaguzi huo ambapo Museveni analenga kutetea wadhifa wake baada ya kuwa madarakani tangu 1986. Anawania kupitia chama tawala cha NRM.

Mwanasiasa msanii Robert Kyangulanyi maarufu kama Bobi Wine naye atakuwa akijaribu bahati yake kwa mara ya pili baada ya kupoteza kwa Museveni miaka mitano iliyopita (2021).

Wine amejizolea umaarufu mkubwa miongoni mwa vijana na anawania kupitia NUP. Katika uchaguzi wa 2021 alipata asilimia 35 ya kura zilizopigwa.

Jijini Kampala hali ya usalama imeimarishwa huku magari ya kijeshi na wanajeshi wenyewe wakishika doria katika barabara mbalimbali.

Hakujawahi kuwa na upokezanaji wa mamlaka Uganda tangu taifa hilo lijinyakulie uhuru mnamo 1962.

Baadhi ya raia wametilia shaka uwazi kwenye kura hiyo wakisema utakuwa tu unaendeleza utawala wa Museveni.

“Katika historia, hakuna uchaguzi ambao umewahi kuwa huru kwa sababu Museveni anatumia ukora tu kupata ushindi,” akasema Opolot Jerome.

“Sasa hakuna intaneti na upigaji kura unatarajiwa kuendelea kwa kutumia mashine na teknolojia ya kisasa. Hiyo itawezekana aje?” akauliza Maria Teremwa.

“Kampeni yenyewe imekuwa ya fujo, wafuasi wa upinzani wanapigwa. Sioni kama wengi watajitokeza kushiriki kura,” akaongeza Taremwa.

Alipokamilisha kampeni zake mnamo Jumanne, Wine ambaye alikuwa amevalia fulana na helmeti ya kujikinga, aliwataka vijana washiriki uchaguzi na kulinda kura zao.

Misafara ya kampeni ya Wine, 43, imekuwa ikiandamwa na fujo, akirushiwa vitoza machozi, wafuasi wake wakinyakwa na polisi kumwekea vizuizi barabarani.

Katika uchaguzi mkuu wa 2021, ghasia zilizuka ambapo zaidi ya watu 50 walikufa huku mamia ya wafuasi wa Wine wakinyakwa jijini Kampala.

Museveni katika kampeni zake amekuwa akijisifia kwa kuleta utulivu na udhabiti Uganda huku akiahidi kuendelea kutekeleza miradi ya maendeleo.

Wine naye amekuwa akiahidi mabadiliko, akisema utawala wa Museveni umechangia umaskini mkubwa nchini humo.