Uhuru apigwa kumbo, aambiwa aachie Gachagua usemaji wa Mlima siasa za 2027
WANDANI wa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua sasa wamemtelekeza Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta wakishikilia kuwa wanamtambua mbunge huyo wa zamani wa Mathira kama kigogo wa Mlima Kenya kuelekea 2027.
Wamesema kwa sababu ameondoka mamlaka Bw Kenyatta anafaa kuwa mshauri wa viongozi wa sasa wala sio msemaji wao katika masuala ya siasa.
“Sisi yule tunayemtambua hapa Mlima Kenya ni Gachagua. Yeyote anayetaka kuungana nasi sharti afanye hivyo kupitia kwake. Uhuru ambaye sasa amestaafu atasalia tu kuwa mshauri wetu wala sio msemaji wetu,” akasema Seneta wa Murang’a Joe Nyutu, wakati wa Ibada ya Kanisa la AIPCA, Kihoya, lililoko eneo bunge la Mathioya, Kaunti ya Murang’a.
Ibada hiyo pia ilihudhuriwa na Bw Gachagua ambaye ndiye kiongozi wa kitaifa wa chama cha Democracy of the Citizens Party (DCP).
“Yeyote ambaye anataka kupata uungwaji mkono kutoka watu wa Mlima Kenya sharti apitia Rigathi Gachagua. Yeye ndiye ufunguo wa kuingia mlimani sasa wala sio Uhuru,” Bw Nyutu akasisitiza.
Kauli hiyo ilionekana kuungwa mkono sio tu na Bw Gachagua mwenyewe, bali wakereketwa wengine wa DCP waliohudhuria ibada hiyo kama vile Mbunge wa Embakasi Kaskazini James Gakuya na aliyekuwa Mbunge wa Kigumo Jamleck Kamau.
Kwa misingi hiyo, wanasiasa hao walimwonya aliyekuwa Waziri wa Usalama wa ndani Bw Fred Matiang’i akome kuongozwa na katibu mkuu wa chama cha Bw Kenyatta, Jubilee, Jeremiah Kioni.
“Bw Kenyatta alihudumu kama Rais kwa kipindi cha miaka 10 na akastaafu. Hatufai kuwa na taswishi kuhusu ni nani anafaa kutupa mwelekeo wa 2027 kama jamii. Kiongozi wetu wa kisiasa sasa ni Bw Gachagua na yeyote anayeletwa hapa Mlimani kupitia mtu mwingine amepotea njia,” seneta Nyutu akakariri.
Kwa upande wake, Bw Gakuya alalamikia kile alichokitaja kama njama ya Rais William Ruto ya kuwagawanya kwa misingi ya kisiasa wakazi wa Mlima Kenya akisema zitafeli.
“Vile vile, kuna wale wanaoendelea kutuambia kuwa eti tunapasa kusubiri mwelekeo kuhusu siasa za 2027 kutoka kwa Bw Kenyatta ilhali Rigathi yuko. Hao ni watu wanaotaka kuturudisha nyuma,” akaongeza.
Bw Gakuya alisema kwamba kile “watu kama hao” wanafaa kujua ni kwamba sasa Bw Kenyatta ni rais mstaafu.
“Tuwe na msimamo thabiti kuhusu siasa za 2027. Hakuna mahali ambapo tunategemea kauli ya Rais mstaafu. Sisi tuko nyuma ya Gachagua na chama chetu ni DCP,” Bw Gakuya akakariri.
Mbunge huyo alimtaka Dkt Matiang’i akome kufuatafuata Bw Kioni akisema anapoteza wakati wake iwapo hatajumuika na Bw Gachagua kama msemaji wa Mlima Kenya.
Naye Bw Kamau alimtaka Bw Kenyatta apumzike na ampishe Bw Gachagua kuongoza jamii za Mlimani katika mapambano ya kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
“Mimi nilikuwa mshirika mkuu wa Bw Kenyatta na nilikuwa nikiwania ugavana wa Murang’a. Nilipewa vitita vya pesa nimwage Murang’a na nilifanya hivyo kwa roho moja. Lakini wapiga kura walinikataa licha ya kutia mifukoni pesa zangu,” akasema.
Alisema kwamba kwa sasa ameamua kutofuata Bw Kenyatta na badala yake ajiunge na Bw Gachagua aliye na sauti ya wapiga kura wa Mlimani.
“Mimi ningetaka kuwashauri Rais Ruto na Naibu wake Kithure Kindiki ambao kwa sasa wanazunguka wakimwaga pesa kwa watu wetu. Mbinu hiyo haikutufaa tukiwa na Bw Kenyatta. Walikula pesa zetu na hatimaye tukakataliwa. Tuulize sisi na ndio sababu nimeamua kujiunga na sauti ya Mlima ambayo ni Gachagua,” akasema.
Bw Gachagua pia alizungumzia njama inayoendeshwa ya kugawanya wakazi wa Mlima Kenya kwa misingi kaunti wanakotoka.
“Nataka nimwambia Rais Ruto kwamba mbinu hiyo ya kuhakikisha kuwa kila kaunti katika Mlima Kenya inatoa mgombea urais itafeli kwa sababu wakazi wameungana nyumba ya chama chetu cha DCP,” akaeleza.
Mbunge huyo wa zamani wa Mathira alisema jukumu kuu alilo nalo sasa ni kupalilia umoja wa Mlima Kenya na kutokomeza kabisa chama cha United Democratic Alliance (UDA).
“Kazi yangu ni ya kubomoa urais huu wa Ruto ambao nilisaidia kuujenga. Pia, Niko na jukumu la kuwa kiongozi wa kupinga kuchaguliwa kwa wasaliti wa kijamii. Aidha, niko na kibarua cha kukuza viongozi chipukuzi wa kutufaa kwa mîaka 30 ijayo. Msingi ninaoweka wa kisiasa ni wa kutudumisha kama jamii kwa mîaka 100 ijayo,” akasema.
Ili afanikiwe, Bw Gachagua alisema anahitaji uungwaji mkono kama msemaji wa Mlima na aaminiwe kutoa mwelekeo wa kipekee kuhusu 2027.
Kauli ya mwanasiasa huyu inakinzana na ile aliyotoa mapema mwaka huu ambapo alishikilia kuwa Bw Kenyatta bado angali msemaji wa kisiasa wa eneo la Mlima Kenya.