Upinzani walaani utumizi wa wahuni kuvuruga mikutano wakionya kwamba ‘raia watajikinga’
MUUNGANO wa Upinzani umeonya dhidi ya wahuni kutumika kuvuruga mikutano yao ya kisiasa, ukisema kuwa hatua hiyo inaweza kutumbukiza nchi katika machafuko.
Viongozi hao wamemtaka Rais William Ruto kuingilia kati na kukomesha vitendo hivyo mara moja, wakisisitiza kuwa haki ya wananchi kushiriki siasa kwa amani haiwezi kuzimwa kwa vitisho au vurugu.
Onyo hilo linafuatia vurugu zilizoshuhudiwa Jumatatu katika eneo la Gusii, ambapo kundi la watu wanaodaiwa kuwa wahuni waliokuwa na panga, rungu na silaha nyingine butu walivamia miji ya Kisii na Keroka wakilenga kuvuruga mikutano ya upinzani.
Wananchi walijibu kwa kuwakabili na kufanikiwa kuwanyang’anya baadhi yao silaha, huku kadhaa wakijeruhiwa, wengine vibaya, kabla ya hali kurejea kawaida.
Katika mkasa huo, gari aina ya Probox linalodaiwa kutumiwa na wahuni lilichomwa moto huko Keroka, huku lori la chama cha Jubilee likiharibiwa pamoja na mali nyingine.Mamia ya wakazi baadaye walivamia Uwanja wa Gusii wakitaka wahutubiwe kutoka hapo.
Jumatatu jioni, moto ulizuka katika mojawapo ya ofisi na kuteketeza zulia na fanicha, lakini viongozi wa upinzani walidai huenda ulianzishwa makusudi na wapinzani wao.
Ziara ya viongozi hao katika kaunti za Kisii na Nyamira ilianza Jumatatu, na inatarajiwa kukamilika Jumatano.
Jana walihutubia mikutano Nyamira Mjini na Marani, kabla ya kuelekea Nyakoe, Suneka na Nyamarambe. Viongozi hao walikuwa wageni wa mgombea urais wa Jubilee, Dkt Fred Matiang’i.
Waliozungumza na wanahabari ni pamoja na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, aliyekuwa Makamu wa Rais Kalonzo Musyoka, aliyekuwa Waziri Eugene Wamalwa na kiongozi wa PNU Peter Munya.
Dkt Matiang’i alilaani vikali vurugu hizo akisema ni jambo la kusikitisha kuona maisha yakipotea kwa sababu za kisiasa.
“Hatuwezi kupoteza maisha kwa sababu ya siasa. Tofauti za kisiasa hazimaanishi uadui,” alisema, akiongeza kuwa ni sharti viongozi wakubali mazungumzo, kuzungumza kwa heshima na kuheshimu maoni tofauti.
Alisisitiza kuwa vijana waliohusika katika vurugu hizo walitolewa nje ya Kisii na Nyamira, jambo linaloashiria matumizi makusudi ya wahuni kwa malengo ya kisiasa.
Bw Gachagua alidai kuwa maafisa wa polisi wanashinikizwa kuruhusu wahuni kuvuruga mikutano yao, akionya kuwa hatua hiyo inaweza kutumbukiza nchi kwenye machafuko ikiwa wananchi wataamua kujilinda.
Alisema, “kujilinda binafsi kumekubaliwa kikatiba na wananchi wa Keroka na Kisii walijilinda wenyewe dhidi ya wahuni. Wakenya wengine wanapaswa kuiga mfano huu.”
Naye Bw Kalonzo alisisitiza kuwa ni jukumu la serikali kuhakikisha usalama wa wananchi wote bila ubaguzi wa kisiasa.
Alionya kuwa ghasia za kisiasa zinadhoofisha misingi ya demokrasia na akaitaka serikali kuheshimu haki ya kikatiba ya mikutano ya kisiasa.
Viongozi hao pia waliwataka wananchi kutokuwa na hofu, kushiriki mikutano ya kisiasa kwa amani, na kudumisha utu, heshima na mazungumzo badala ya vurugu.
Wamehimiza idara za usalama kuchunguza visa vya vurugu na kuhakikisha waliohusika wanachukuliwa hatua za sheria, huku wakisisitiza kuwa Kenya ni mwanachama wa Mkataba wa Roma na Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai ili kuhakikisha kuwa haki na amani ya wananchi inadumishwa.