Habari za Kitaifa

Utata wa Idd waibuka tena mfungo wa Ramadhani ukitamatika

Na FATUMA BUGU March 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUKU mwezi mtukufu wa Ramadhani ukitamatika, tofauti za kuandama kwa mwezi zimejitokeza na kusababisha sikukuu ya Idd-ul-Fitr kusherehekewa siku tofauti miongoni mwa Waislamu.

Baadhi ya waumini hao wanasema Eid itakuwa leo Alhamisi huku wengine wakitaja siku ya Ijumaa au hata Jumamosi.

Wale watakaoanza kutazama mwezi jioni ya jana, Jumatano ni wale walioanza kufunga mapema ya Februari 18, 2026, wakifuata mwandamo wa mwezi wa kimataifa badala ya tangazo rasmi la kaimu Kadhi Mkuu wa Kenya, Sheikh Sukyan Omar lililotolewa 19 Februari 2026.

Hata hivyo, viongozi wa dini pamoja na wananchi wanasisitiza umuhimu wa umoja na heshima licha ya tofauti hizo.

Kwa mujibu wa Sheikh Omar Buya, tofauti hizi zinatokana na mitazamo miwili mikuu kama mwandamo wa mwezi wa kimataifa na mwandamo wa ndani wa maeneo husika.

“Tofauti hizi zinahusiana na Hadithi ya Mtume Muhammad (rehema na amani zimshukie) inayosema kuwa fungeni mtakapouona mwezi na fungueni mtakapouona.

“Hivyo, baadhi ya Waislamu wanaamini mwezi ni mmoja dunia nzima na unapaswa kufuatwa kimataifa, huku wengine wakiamini kuwa kufunga na kufungua kunapaswa kuzingatia muandamo wa mwezi katika maeneo yao,” alisema Sheikh Buya.

Kwa mujibu wa mwongozo kutoka kwa Fatwa Council of Kenya, mwezi mwandamo wa Shawwal ambao ni mwezi wa kumi katika kalenda ya Kiislamu unaofuata baada ya Ramadhani utaangaliwa katika nyakati tofauti, ambapo baadhi ya Waislamu wataanza kuutafuta Jumatano na wengine Alhamisi.

Wanazuoni wanasema kuwa tofauti hizi zina msingi halali katika fiqhi ya Kiislamu na hazipaswi kuwa chanzo cha mgawanyiko.

Mwenyekiti wa Pwani Patriotic Religious Leaders, Sheikh Abu Qatada Namisi, aliwahimiza Waislamu kuzikubali tofauti hizi kwa uelewa.

Baadhi ya Waislamu wanasema kuwa tofauti hiyo haijalishi muhimu ni mavuno ya Ramadan na kukubalika kwa ibada.

“Haijalishi watu watasherehekea Alhamisi, Ijumaa au Jumamosi. Mradi ni Idd, tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumalizika kwa Ramadhani. Tunaomba ibada zetu zikubaliwe na tuendelee kufanya mema,” alisema Mohammed Abdallah, mkazi wa Mombasa.

Kwa mujibu wa Kenya Fatwa Council, shughuli ya kuandama mwezi itafanyika Alhamisi, Machi 19, jioni ili kubaini siku ya mwisho ya Ramadhani na mwanzo wa Idd-ul-Fitr katika Afrika Mashariki.

Katika taarifa yao rasmi, mwenyekiti wa baraza hilo, Sayyid Ahmad Ahmad Badawy, alisema takwimu za kisayansi na ripoti kutoka vituo maalum vya ufuatiliaji wa mwezi zinaonyesha kuwa haitawezekana kuuona mwezi huo jioni ya Alhamisi katika Afrika Mashariki.

“Hivyo basi Ramadhani itakamilishwa kuwa siku 30, na kufunga kutaendelea Ijumaa, Machi 20, 2026, ambayo itakuwa siku ya mwisho ya Ramadhani katika Afrika Mashariki. Kwa hivyo, Jumamosi, Machi 21, 2026, itakuwa siku ya kwanza ya Idd-ul-Fitr,” alisema.

Ofisi ya Kadhi Mkuu tayari imealika taasisi na mashirika kuteua wawakilishi wao kushiriki katika zoezi la kitaifa la kuandama mwezi litakalofanyika Alhamisi, Machi 19, ambayo ni usiku wa 29 Ramadhani.

Viongozi wa dini pia wameeleza kuwa iwapo mwezi hautaonekana kwa wale wanaoanza Jumatano jioni, huenda wakasherehekea Idd siku ya Ijumaa baada ya kukamilisha siku 30 za kufunga.

Licha ya tofauti hizi, wanazuoni wanasema hali kama hii imekuwepo kwa muda mrefu katika Uislamu na inatambuliwa kisheria.

Badala ya kusababisha mgawanyiko, tofauti hizi zinatoa fursa ya kuimarisha umoja kupitia uvumilivu na imani ya pamoja.

Katika siku hii, Waislamu wanahimizwa kutoa Zakatul Fitr, sadaka ya lazima inayolenga kutakasa mfungaji na kuwasaidia wahitaji.

“Zakatul Fitr si ibada ya kawaida tu, bali ni njia ya kuhakikisha kila mtu, bila kujali hali yake, anaweza kusherehekea Eid kwa heshima. Kila Muislamu mwenye uwezo anapaswa kutoa kwa niaba yake na wale walio chini ya uangalizi wake,” alisema Sheikh Buya.

Sadaka hii kwa kawaida hutolewa kwa vyakula kama mchele, ngano, tende au mahindi, kwa kiasi cha kilo 2.5 hadi 3 kwa kila mtu. Pia muislamu anaweza kutoa chakula au pesa.