Vijana katika mradi wa serikali ‘Kazi Majuu’ wabaki hoi kugundua kuna ada za siri
HUENDA mamia ya vijana kutoka Pwani wakakosa kusafiri kwa kazi za serikali Dubai kutokana na ada za siri za matibabu na uthibitishaji wa stakabadhi ambazo wanadai hazikutajwa walipofahamishwa kuhusu mpango huo.
Katika mahojiano na Taifa Leo, vijana hao wanaotafuta kazi katika mpango wa serikali wa “Kazi Majuu” walisema walivutiwa na ahadi kuwa serikali ingeshughulikia gharama zote kupitia Hazina ya Vijana na kisha kukata kiasi hicho kutoka mishahara yao pindi watakapoanza kazi.
Hata hivyo, hali imebadilika ghafla huku wengi wakitakiwa kulipa hadi Sh30,000 kabla ya kuondoka. Mbwana Ali, 24, kutoka Shimoni, Lunga Lunga, Kaunti ya Kwale, ni miongoni mwa walioathiriwa.
Bw Ali, ambaye alihitimu kidato cha nne na sasa hana ajira, alisema alishindwa kuripoti Nairobi Juni 9, kama alivyoagizwa baada ya kutakiwa kulipa ada hiyo kubwa.
“Niliambiwa Sh30,000 ni za uchunguzi wa afya na uthibitisho wa stakabadhi. Hii sivyo tulivyoambiwa awali. Tuliahidiwa fedha hizo zingelipwa na serikali kupitia mkopo wa Hazina ya Vijana,” alisema Bw Ali.
Alieleza kuwa alikuwa ameweka matumaini yake yote kwenye kazi hiyo kama njia ya kujikwamua kutoka kwa uchochole.
“Nilikusudia kufanya kazi kwa miaka mitano hadi minane, nijikusanyie mtaji na nirudi nyumbani kuanzisha biashara ya kilimo,” alisema kwa huzuni.
Kwa upande mwingine, Mwangi David kutoka Matuga alisema alilazimika kukopa Sh130,000 za visa, mbali na Sh7,500 kwa uchunguzi wa afya na Sh6,000 kwa stakabadhi.
“Tuliambiwa KCB itatupatia mikopo bila dhamana, lakini walitutaka tuwe na mdhamini au hati ya ardhi. Baadaye tukaelekezwa kwa Hazina ya Uwezo lakini hadi sasa hakuna fedha yoyote tumepata,” alisema Bw Mwangi.
Bw Mwangi, 27, sasa anahangaika jinsi ya kulipa mkopo huo baada ya kusubiri kwa miezi miwili bila maelezo ya lini atasafiri.
“Ajenti hawapokei simu zetu. Ukiingia mtandaoni, visa inaonyesha iko kwenye mchakato lakini hakuna taarifa rasmi. Sijui nisubiri au niache kabisa,” alisema.
Maafisa wa serikali walitangaza kuwa zaidi ya vijana 4,000 wataajiriwa kupitia mpango huo wa “Kazi Majuu” unaoendeshwa na Wizara ya Leba na Ulinzi wa Jamii.
Mpango huo ulilenga kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana kwa kuwapeleka kufanya kazi katika Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Taifa Leo ilipowasiliana na ajenti mmoja wa uajiri kutoka kampuni ya Zawadi International, afisa mmoja aliyeomba kutotajwa jina alisema Sh30,000 ni za uchunguzi wa afya.
“Serikali inagharimia visa na tiketi ya ndege pekee. Gharama ya uchunguzi wa afya ni lazima, maana hatuwezi kupeleka mtu ambaye hana afya nzuri kufanya kazi,” alisema.
Kauli hiyo hata hivyo imepingwa na viongozi wa vijana ambao wanasema wenzao walidanganywa.
“Tumepokea malalamishi mengi ya vijana kudaiwa Sh30,000 kabla ya kusafiri. Hii ni kinyume kabisa na ahadi ya serikali kuwa gharama hizo zingelipwa kupitia mikopo ya Hazina ya Vijana,” alisema Bw Mbwana Omar, Rais wa Bunge la Vijana Kaunti ya Kwale.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari, Bw Omar alisema tayari amewasiliana na Mbunge wa Msambweni, Bw Feisal Bader, kutaka ufafanuzi kuhusu ada hiyo mpya.
“Hadi sasa hakuna majibu rasmi kutoka kwa ofisi ya mbunge. Tumeamua kuwataka vijana wasiende Nairobi wala kulipa fedha yoyote hadi serikali itoe kauli rasmi. Afya na usalama wa vijana ni muhimu,” alisema.
Waziri wa leba Bw Alfred Mutua alisema serikali itagharamikia tiketi ya ndege na visa pekee.
“Hazina ya vijana haiwezi kulipia uchunguzi wa matibabu,je ukipatikana hauna afya nzuri kufanya kazi nani atalipi?” akauliza.
Aliongezea kuwa vijana wanapaswa kujikakamua kulipa ada ya matibabu.
“Serikali itakulipia zaidi Sh200,000, gharama ya usafiri na visa, unaweza kushindwa kutafuta Sh15,000 pekee? Kama huwezi utakuwa unadhihaka hatukutaki,” akasema.
Juhudi za kumpigia mbunge wa Msambweni Feisal Bader hazikufua dafu.
Katika Kaunti ya Kilifi, Bw Daniel Jefwa aliitaka serikali kutoa maelezo ya wazi kuhusu mchakato huo wa uajiri.
“Mpango huu unaleta matumaini makubwa kwa vijana lakini sasa unageuka kuwa chanzo cha matatizo. Serikali inapaswa kusema ukweli na kuwa wazi kuhusu gharama halisi,” alisema.
Wakati serikali inaonekana kimya, maelfu ya vijana waliojiandikisha wakitumai maisha bora sasa wanakumbwa na wasiwasi, madeni na sintofahamu kuhusu hatima ya ndoto zao.