Habari za Kitaifa

Waathiriwa wa maandamano kufidiwa Juni, Rais atangaza akisema ametenga Sh2 bilioni

Na CECIL ODONGO March 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto, jana alisema kuwa wahanga wa maandamano nchini watalipwa fidia kufikia Juni mwaka huu huku Sh2 bilioni zikitengewa shughuli hiyo kwenye Bajeti ya ziada ya 2025/26.

Rais alisema mchakato wa kuwatambua wanaostahili fidia hiyo umekamilishwa, na Mamlaka Huru ya Kutathmini Utendakazi wa Polisi (IPOA) pamoja na Tume ya Kitaifa ya Kutetea Haki za Kibinadamu (KNCHR).

“Ni imani yetu kwamba tutamaliza suala hilo kufikia Juni kama hakuna chochote ambacho kitatokea,” akasema Rais Ruto.

Alikuwa akiongea jana katika ukumbi wa KICC, wakati wa mkutano wa Kundi la Wabunge wa UDA na ODM.

Mkutano huo ulikuwa wa kutathmini utekelezaji wa Ajenda 10 ambazo zilikuwa kwenye muafaka kati ya Rais Ruto na marehemu Kiongozi wa ODM Raila Odinga. Makubaliano hayo yalitiwa saini mnamo Machi 7, 2025.

Mkutano wa jana pia ulihudhuriwa na Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki, Kinara wa ODM Dkt Oburu Oginga na wabunge ambao wanaunga mkono Serikali Jumuishi.

“Huwezi kufidia maisha yaliyopotea, lakini unaweza ukafanya jambo. Hii ndiyo maana tulichukua hatua ya kwanza ambayo ni kuchapisha majina ya wanachama wa jopo la fidia lakini suala hilo likaishia mahakamani,” akaongeza Rais.

Wahanga wa maandamano ambao watanufaika ni wale walishiriki maasi hayo baada ya uchaguzi wa 2017 na 2022 na wakati wa maandamano ya Gen Z mnamo 2024.

“Tumewatambua manusura kupitia KNCHR na IPOA na orodha hiyo inaanzia 2017. Wabunge sasa wana kazi ya kuidhinisha Sh2 bilioni za kufanikisha malipo hayo,” akasema Dkt Ruto.

Mchakato huo hapo awali ulikuwa ukikabiliwa na vizingiti vya kisheria lakini mahakama ilitoa mwongozo wa kulipwa kwa fidia.

Wiki jana, serikali ilichapisha majina ya wanachama wa jopo la kuongoza ulipaji wa fidia hiyo.

Kando na fidia, Rais pia alisema serikali inamakinika kuhakikisha kwamba waandamanaji wanalindwa ili kusizuke ghasia na maisha kupotea siku zijazo.

“Hatukomi hapa bali tunaangalia mbele kwa sababu maandamano ni haki ya Wakenya na lazima walindwe.

Serikali haitakuwa mstari wa mbele kuibuka na sheria mpya ya kuongoza maandamano kwa sababu huo ni mgongano wa majukumu,” akasema Rais.

Katika ripoti iliyosheheni hatua zilizopigwa katika kutekelezwa kwa Ajenda10, ilibainika kuwa IPOA imeshughulikia kesi 820 za dhuluma za polisi ambapo maafisa 49 wamehukumiwa katika kesi 35.

Aidha Mswada ambao ulikuwa upendekezwa kudhibiti maandamano nao ulitolewa, huku Wizara ya Usalama wa Ndani ikitoa sera zinazowazuia polisi kutumia nguvu kupita kiasi wakati wa maandamano.

Viongozi wa upinzani na wale waasi ndani ya ODM wamekuwa wakitumia suala la ulipaji fidia kusawiri maelewano kati ya Rais na marehemu Raila, kama jambo ambalo halikuheshimiwa.