Habari za Kitaifa

Wabunge watishia kuondoa Hazina ya Usawazishaji Maendeleo inayopeleka fedha zaidi maeneo yaliyotengwa

Na ERIC MATARA March 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WABUNGE sasa wanatishia kuondoa Hazina ya Usawazishaji wa Maendeleo wakisema haijachangia kwa vyovyote kuinua kaunti ambazo zimebaguliwa kwa miaka mingi na tawala zilizopita.

Chini ya Katiba Mpya ya 2010, Hazina hiyo ilikuwa ifanye kazi hadi 2030 na Bunge lilipewa mamlaka ya kuongeza muda wake kutegemea ufanisi wake.

Hata hivyo, baadhi ya wabunge sasa wanataka hazina hiyo iondolewe kwa sababu tangu ianzishwe, hazina hiyo haijapokea Sh62.7 bilioni kutoka Hazina Kuu ya Fedha.

Afisa Mkuu Mtendaji wa Hazina ya Usawazishaji wa Maendeleo Guyo Boru alithibitisha kuwa wanadai deni hilo.

“Hatujapokea pesa hizo jinsi ambavyo inatakikana kisheria,” akasema Bw Boru.

Kaunti ambazo zinastahili kunufaika ni Samburu, Turkana, Mandera, Baringo, Pokot Magharibi, Wajir, Garissa kati ya nyingine ambazo zilikuwa zimetelekezwa na serikali kuu zilizopita kwa miaka mingi.

Kila mwaka, asilimia 0.5 ya mapato ya serikali yanastahili kuelekezwa katika hazina hiyo.

Hata hivyo, kando na kucheleweshwa, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali amebaini kuwa pesa zilizotolewa hazijatumika vizuri, mara nyingi zikiishia kuporwa.

Bw Boru alipofika mbele ya Kamati ya Uwiano na Nafasi sawa alisema kuwa hazina hiyo haina matokeo ya kujivunia kwa sababu jamii tengwa zimesalia bila huduma muhimu.

Malengo

“Hazina ya Usawazishaji wa Maendeleo haijatimiza malengo yaliyokusudiwa. Jamii tengwa zilikuwa na matumaini lakini hadi sasa hakuna chochote kilichofanyika,” akasema Mwenyekiti wa Kamati ya Uwiano na Nafasi sawa Adan Yusuf Haji (Mbunge wa Mandera Mashariki).

Bw Haji alisema kuwa hata pesa ambazo zimetumwa kwa hazina hiyo hazijatumika kuyabadilisha maisha ya raia kupitia miradi mbalimbali iliyokumbatiwa.

Naibu Mwenyekiti wa kamati hiyo Duncan Mathenge (Mbunge wa Nyeri) aliwakashifu wasimamizi wa hazina hiyo kwa kuanzisha miradi mingi kisha kukosa kuikamilisha.

“Miradi mingi kwa mfano katika Kaunti ya Narok imekwama baada ya pesa za umma kutumika. Inashangaza kuwa wabunge wamekuwa wakitengwa katika kuamua miradi ya kutekelezwa kupitia hazina hii,” akasema Bw Mathenge.

Mbunge wa Narok Kaskazini Agnes Pereiyo naye alisema kuwa jamii ya eneobunge lake ilikuwa na matumaini kwenye ufanisi wa hazina hiyo lakini sasa imekata tamaa.

“Hizi hazina ipo tu kwenye karatasi na kama viongozi kutoka maeneo tengwa, hatujaona miradi ambayo hazina hii ilifadhili na kufanikisha,” akasema Bi Pareiyo.

Mbunge wa Eldas Adan Keynan alisema hazina ni silaha tu ya kisiasa bila athari za kimaendeleo kwa jamii.

“Hakuna usawa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na sasa inatumika na serikali kuwatunuku wanasiasa waaminifu au kuadhibu wasiokubaliana utawala wa sasa. Licha ya uwepo wa hazina hii, kaunti nyingi za Kaskazini mwa Kenya bado hazina mahitaji ya kimsingi kama maji na afya,” akasema Bw Keynan.