Habari za Kitaifa

Wadau wa utalii walia Pasaka imefika mapema ikigongana na wiki ya kufunga shule

Na WINNIE ATIENO April 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SEKTA ya utalii katika eneo la Pwani, imeathiriwa na jinsi Pasaka imefika mapema, ikifanyika karibu wakati mmoja na kufungwa kwa shule.

Familia nyingi zilikuwa zikipata muda wa kutosha kufanya maandalizi ya safari za kusherehekea Pasaka pamoja na mapumziko ya Aprili wakati Pasaka ikiwa katikati ya mwezi.

Hata hivyo, mwaka huu, Pasaka imeangukia ndani ya wiki ile ile ya kufungwa kwa shule, jambo linalosababisha muda mdogo wa kupanga safari.

Meneja Mkuu wa Hoteli ya Plaza Beach Mombasa, Bw Dennis Gwaro, alikiri kuwa wanapoingia katika kipindi ambacho kawaida ni mojawapo ya vipindi vya shughuli nyingi zaidi kwa hoteli, wiki ya Pasaka mwaka huu inatoa fursa nzuri pamoja na changamoto za kiutendaji kwa mpigo.

Kwa wageni wengi, hasa watalii wa ndani ya nchi, ratiba za shule ndizo hutoa mwongozo wa kupanga likizo.

Wakati tarehe hizi zinapobadilika au kukaribiana sana, mipango ya safari huwa ni changamoto kwa vile lazima yafanywe ndani ya muda mfupi.

“Tumebaini hili wazi kupitia jinsi wageni wanataka kuhifadhi vyumba. Mahitaji ya kutalii kwa hakika yapo; hamu ya kusafiri kwenda Mombasa bado iko juu. Hata hivyo, tunaona muda mfupi wa kuhifadhi vyumba, idadi kubwa ya watu wanaulizia, lakini hawafanyi maamuzi ya haraka,” akasema.

“Kwa kuwa safari zinataka kufanywa dakika za mwisho, ndege, treni na njia nyingine za usafirishaji zimejaa. Hii inaathiri moja kwa moja hoteli zetu. Hata pale ambapo mahitaji ya vyumba yako juu, ukosefu wa usafirishaji ni kizuizi,” alisema.

Afisa wa Chama cha Wahudumu wa Hoteli (KAHC) tawi la Pwani, Dkt Sam Ikwaye, alisema Aprili bado ni kipindi cha kilele kwa sekta ya utalii na wanatarajia matokeo bora zaidi ndani ya mwezi.

Kwa mujibu wa Dkt Ikwaye, hoteli nyingi katika eneo hili kwa sasa zina kiwango cha wastani cha asilima 70 cha uhifadhi wa vyumba.

“Pwani bado ni eneo la familia kutalii, na kufungwa kwa shule kunatoa fursa kwa familia nyingi kusafiri,” alisema.

Kaimu Mwenyekiti wa Chama cha Utalii Pwani (KCTA) Victor Shitakha, alibainisha kuwa ingawa Pasaka inatarajiwa kuleta ongezeko la wageni, msimu mzima haujakuwa wa kuridhisha, jambo linalosababisha hoteli kuongeza jitihada za matangazo.

Wadau wengine katika sekta ya utalii walieleza matumaini kwamba familia zinachukua nafasi ya likizo ndefu kusafiri.

“Wakati Pasaka inafanyika ndani ya kipindi cha likizo za shule, kawaida tunaona wageni wakikaa kwa muda mrefu na wengi wakihifadhi vyumba, hasa kwa watalii wa ndani,” alisema Meneja Mkuu wa Hoteli ya Bamburi Beach Michael Otieno.

Alisema mwelekeo wa sasa unaonyesha ongezeko la wanaoulizia nafasi na kuhifadhi vyumba mapema, hasa kutoka kwa familia zinazopanga likizo zao.

Wadau wa sekta wamesihi idara nyingine zote zinazohusika katika kuwezesha utalii, ikiwemo sekta ya uchukuzi na serikali za kaunti, kuhakikisha kuna mazingira bora ya kuwezesha watalii kutotatizika.

Aidha, wamesisitiza kuwa, kuboresha miundomsingi, kuongeza usalama na utoaji wa huduma thabiti itakuwa muhimu katika kudumisha ukuaji baada ya kipindi cha likizo.

Haya yanajiri huku wanafunzi wakirejea nyumbani kwa mapumziko wa mwezi mmoja kabla ya kufungua shule kwa muhula wa pili.