Wafuasi, mahasimu wa ODM wakanganyika, wamuamini nani kati ya Raila na Sifuna?
HATUA ya Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna kuendelea kuushambulia ushirikiano wa kiongozi wa chama hicho Raila Odinga na Rais William Ruto, imeibua mjadala kuhusu mipango ya chama hicho kuhusu uchaguzi wa mwaka wa 2027.
Kwa upande mmoja, seneta huyo wa Nairobi amejisawiri kama mwasi anayelenga kuvuruga ODM akiwa ndani huku kwa upande mwingine akionekana kama anayetumiwa na Bw Odinga kuendeleza mikakati yake ya kujiondoa katika mkataba kati ya ODM na UDA.
Huku Bw Odinga akishikilia kuwa ushirikiano kati yake na Rais Ruto utadumishwa hadi 2027, Bw Sifuna amekuwa akipinga msimamo huo akisema ni “mbaya zaidi.”
Hali hiyo imewashangaza maadui na wandani wa chama hicho cha Chungwa wasijue ni nani kati ya Bw Odinga na Bw Sifuna anayepaswa kuaminiwa.
Seneta Sifuna amekuwa akiikosoa Serikali Jumuishi, inayoshirikisha wanachama watano wa ODM wanaoshikilia nyadhifa za uwaziri, kwa ukatili wa polisi na mauaji ya kiholela miongoni mwa dhuluma nyinginezo.
Katibu huyo mkuu amekuwa akishikilia kuwa ODM haiko serikalini wala haitamuunga mkono Rais Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Nyakati nyingine, Bw Sifuna amekuwa akipiga waziwazi kauli za kiongozi wa chama chake.
“Ushirikiano wetu na serikali ya Kenya Kwanza unatugharimu pakubwa. Unatuumiza kama chama kwa sababu upande wake Rais haujajitolea kutekeleza makubaliano yetu tuliyoafikiana kwenye mkataba wa ushirikiano na ndiyo maana ninasema umekufa,” akasema Bw Sifuna.
“Ningependa Ruto ajue kwamba kuondolewa kwake afisini ni ajenda kuu ya kitaifa. Ndiyo ajenda ya kipekee kwa sababu serikali yake inapinga maadili yaliyoorodheshwa kwenye Katiba. Kwa mtazamo wangu ninaunga mkono kuondolewa kwa Ruto. Hoja ya kumtimua afisini ikiwasilishwa katika seneti, nitaiunga haraka zaidi.”
Seneta huyo alieleza kuwa uamuzi wa kushirikiana na UDA ulifikiwa ili kuzuia kuporomoka kwa taifa hili baada ya maasi ya vijana wa Gen-Z, Juni mwaka jana.
Lakini kulingana na Bw Sifuna, ODM haifai kudumisha ushirikiano huo hadi 2027 kwa sababu UDA imedinda kutekeleza MoU hiyo iliyotiwa saini mnamo Machi 7 mwaka huu.
Alieleza kuwa aliishauri ODM dhidi ya kutia saini mkataba wa ushirikiano na UDA “kwani hatua hiyo ingefuta masuala ambayo ODM imekuwa ikitetea” lakini ushauri wake ulikataliwa.
Wakati wa mahojiano ya kipekee na NTV nyumbani kwake katika mtaa wa Karen, Nairobi, Jumamosi, Bw Odinga alisema uamuzi wa ODM kushirikiana na utawala wa Rais Ruto ulifanywa kwa ajili ya kudumisha uthabiti wa kitaifa.
Alieleza kuwa ushirikiano huo ulifikiwa kutokana na msururu wa maandamano ya kupinga serikali yaliyoongozwa na Gen-Z mwaka jana kiasi cha kulitumbukiza taifa hili katika lindi la machafuko sawa na hali ilivyo Somalia, Haiti au Sudan.
“Tumesema kuwa tuko katika Serikali Jumuishi hadi mwaka wa 2027. Hatukusema kuwa tutafanya kazi na UDA hadi baada ya 2027. Hayo ni masuala ambayo yatajadiliwa wakati ufaao na uamuzi kufanywa na wanachama wa ODM si Raila kama mtu binafsi,” akaeleza Bw Odinga.
Lakini kwa upande wake, Katibu Mkuu Sifuna anashikilia kuwa ODM ikidumisha ushirikiano wake na utawala huu hadi mwaka wa 2027, haitapata nafasi ya kujiandaa kwa uchaguzi mkuu.
Hali hii, akasema, itaikosesha ODM nafasi ya kujiondoa katika serikali iliyopoteza umaarufu na kuelezea wananchi sababu ya kushirikiana na utawala huo.
“Kwa hivyo sielewi ni kwa nini baadhi ya wenzetu wanaona ni bora kuendelea kushirikiana na serikali hii hadi 2027 kinyume na matakwa ya wanachama wengi,” akaeleza Bw Sifuna.