Wahanga 1,224 wa maandamano watuma maombi ya fidia wengi wakiwa waliopoteza riziki
ZAIDI ya wahanga 1,224 wa maandamano wametuma maombi ya kulipwa fidia ya Sh2 bilioni, takwimu za Tume ya Kitaifa ya Kutetea Haki za Kibinadamu (KNHCR) zilizotolewa jana zinaonyesha.
Tume hiyo ilisema waliotuma maombi ni familia za watu waliouawa, walioteswa, waliotekwa nyara na waliopotea kupitia njia tatanishi.
Wahanga wengine ni waliofurushwa na waliodhulumiwa pamoja na waliopoteza mali na njia zao za kupata riziki.
Mwezi uliopita, Rais William Ruto alitangaza kuwa utawala wake unalenga kuhakikisha wahanga wa maandamano wanalipwa fidia kufikia Juni mwaka huu.
Serikali imetenga Sh2 bilioni katika bajeti ya ziada kuwalipa wahanga wa maandamano.
Wahanga wa maandamano kulipwa fidia ni kati ya Ajenda 10 ambazo zilikuwa kwenye muafaka uliotiwa saini na Rais William Ruto na marehemu Kiongozi wa upinzani Raila Odinga mnamo Machi 7, mwaka jana.
Kwenye taarifa, Mwenyekiti wa KNCHR, Bi Claris Ogangah, alisema tume hiyo ishabuni mwongozo wa mashauriano na washikadau mbalimbali wanaojumuisha waathiriwa wa maandamano pamoja na mashirika ya serikali na makundi ya kupigania haki.
Tume hiyo imekuwa ikiandaa orodha ya wahanga ambayo baada ya kuhakikiwa itawasilishwa kwa Rais Ruto.
“Hadi sasa tume imeandaa orodha ya wahanga 1,224 waliodhulumiwa na inahakiki maelezo yao,” akasema Bi Ogangah.
Tume hiyo hata hivyo imeibua utata wa bajeti, ikishutumu Hazina Kuu ya Kifedha kwa kutowasilisha fedha hizo kwa wakati.
“KNHCR haijaweza kuzunguka kote nchini jinsi ilivyokuwa ikinuia kutokana na kukosa kutengewa fedha. Tunaomba Hazina Kuu iwasilishe hela tume ilitengewa na bunge kwa wakati ili KNHCR itekeleze wajibu huu wa kikatiba na pia maslahi ya wahanga wa maandamano yatimizwe,” akaongeza akisisitiza pesa hizo zitasaidia tume kutekeleza wajibu wake ipasavyo.
Wahanga wanahitajika wafike afisi za KNHCR ambazo ziko Nairobi, Kitale, Kisumu, Mombasa, Nyahururu, Wajir, Kajiado, Isiolo na Garissa.
Wanahitajika wawasilishe fomu za P3, za kimatibabu, ripoti za OB na za uchunguzi wa maiti pamoja na stakabadhi nyingine.
Kwa mujibu wa tume, iwapo Sh2 bilioni hazitatoshea, serikali itaongeza hela nyingine kwenye bajeti ya mwaka ujao wa kifedha.
Kwa familia ambazo bado wapendwa wao wamepotea kupitia njia tatanishi, tume itawafikia kufahamu hali halisi.