Habari za Kitaifa

Wahuni wateka jiji huku polisi wakimpiga risasi kichwani muuzaji wa barakoa

Na DANIEL OGETTA, CECIL ODONGO June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

MAGENGE hatari jana yaliteka jiji la Nairobi na kuwakabili waandamanaji waliokuwa wakishinikiza kujiuzulu kwa Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat kutokana na mauaji ya kinyama ya mwalimu na bloga Albert Ojwang’.

Katika kile ambacho kimezidisha ghadhabu miongoni mwa Wakenya, polisi mmoja alimpiga risasi kichwani mwanaume aliyekuwa akiuza barakoa karibu na Jumba la Imenti, barabara ya Moi Avenue.

Mwanamume huyo alikimbizwa hospitali ya Bliss ambako ripoti ya polisi inasema yuko hali mahututi.

Jana mamia ya vijana walikabiliana na polisi katikati mwa jiji wakisaka haki kwa Bw Ojwang’ huku wakimtaka Bw Lagat ajiuzulu kabisa.

Naibu huyo inspekta jenerali wa polisi alituma taarifa mnamo Jumatatu kuwa amejiondoa afisini kwa muda lakini waandamanaji jana walishikilia kuwa lazima ajiuzulu kabisa.

Ilani ya maandamano hayo ilionyesha kuwa, yalistahili kuanza Aga Khan Walk katikati mwa jiji lakini kutokana na kujaa kwa maafisa wa usalama maeneo hayo, vijana walibadili mbinu na kuanzia nje ya jumba la Nation.

Hapo ndipo makabiliano yalichacha zaidi baada ya maafisa wa usalama kuwaandama na kuwarushia vitoza machozi huku milio ya risasi ikitamba hewani.

Shughuli zilisimama katika barabara ya Moi, Kenyatta, Kimathi huku waandamanaji wakikabiliana na maafisa wa usalama, wengine wakipiga nduru na wengine wakiimba nyimbo za uzalendo.

“Haya maandamano hayahusu Ojwang’ pekee bali wote ambao walikufa mwaka jana na wanaoendelea kuteseka kimya kimya,” akasema mmoja wa waandamanaji.

Hata hivyo, kitumbua kiliingia mchanga genge la vijana ambao walikuwa kwenye pikipiki na walikuwa wamejihami kwa rungu na kuvaa barakoa, walipofika kwa kishindo katikati mwa jiji.

Polisi waliwaruhusu vijana hao ambao walikuwa wamepaaza sauti wakisama ‘hakuna maandamano’ kuendeleza ukatili wao bila kuwakabili.

Hapo ndipo ilibidi waandamanaji wapambane na makali ya moshi wa vitoza machozi na wakati huo huo na genge ambalo lilikuwa likiwapiga kuzima maasi yao.

Kilichokuwa ushahidi wa ushirikiano kati ya genge hilo na polisi ni kwamba, hata maafisa wa usalama walisikika wakiwapa maagizo jinsi wangepambana na waliokuwa wakiandamana.

Kwenye barabara ya Koinange, polisi walilazimika kumwokoa kijana mmoja ambaye alishukiwa kuwa sehemu ya genge hilo baada yake kupigwa na wahudumu wa bodaboda katikati mwa jiji.

Aliokolewa na mwanaume mmoja raia ambaye alisema hakuwa sehemu ya genge lililokuwa likipambana na raia jijini. Hata pikipiki ambayo ilikuwa ikishukiwa kutumiwa na genge hilo iliteketezwa moto na waandamanaji waliojawa na ghadhabu.

Katika barabara ya Moi Avenue, genge hilo liliendelea kushiriki uhalifu huku wakivunja milango ya maduka ya elektroniki na kuendeleza uporaji polisi wakitazama tu bila hatua zozote zile.

Kwenye video moja iliyonaswa katika barabara ya Koinange, genge hilo bila huruma walimvamia mwanaume moja aliyekuwa amevalia suti na tai akitembea na wakamwangusha chini.

Wakiwa zaidi ya wanne, walimpiga huku wakimpora japo mwanaume huyo alijikakamua na kujaribu kupambana nao lakini akalemewa.

Baada ya kumpora kiasi cha kurarua longí yake, waliabiri pikipiki yao na kuendelea kuwapora wengine huku wakionekana kutotetereka katika kuendeleza uhalifu mchana peupe.

Kisa cha mwanaume muuzaji wa barakoa kupigwa risasi kichwani peupe mchana na polisi aliyekuwa amejihami, kilizua ghadhabu zaidi mitandaoni, wengi wakitaka hatua kali ichukuliwe dhidi ya polisi huyo.

Mwanaume huyo aliyevalia nguo ya samawati na kubeba barakoa wala hakuwa amejihami au kuwa hatari kwa maafisa wa usalama, alipigwa risasi kichwani huku polisi aliyempiga akionekana kutotetereka.

Genge kuingilia maandamano ni jambo ambalo limekuwa likikashifiwa na mashirika ya kupigania haki huku kundi hilo likisababishia wafanyabiashara hasara na kuwajeruhi waandamanaji.

Mwaka jana, wahuni ambao walikuwa wamejihami walishirikiana na polisi waliovalia kiraia na wengine wenye sare kuwakamata vijana wakati wa maandamano ya Gen Z.

Wiki iliyopita, vijana waliodaiwa kukodishwa na mwanasiasa mmoja wa Nairobi walichoma magari wakati wa maandamano, tukio ambalo lililenga kuwasawiri walioandamana kama wahuni.

Mnamo Januari 2021, aliyekuwa Gavana wa Nairobi Mike Sonko alizua mdahala mtandaoni baada ya kudai walinunua magari makukuu kisha kuyateketeza kusawiri wafuasi wa ODM kama wahuni wakati wa maandamano mnamo 2017.

Bw Sonko alidai kuwa walishiriki mpango huo pamoja na aliyekuwa Katibu katika Wizara ya Usalama wa Ndani Karanja Kibicho na wengine japo Bw Kibicho alikanusha hilo na hata kuwasilisha malalamishi kuhusu kauli hiyo kwa Idara ya Upelelezi Nchini (DCI).

“Nataka kutubu na kusema kuwa mnamo 2017, wakati ODM ilikuwa ikiandaa maandamano Nairobi, mimi pamoja na Kibicho na washirika serikalini tulichapisha fulana zinazofanana na za ODM na kununua magari makukuu. Tuliyateketeza magari hayo kwenye barabara ya Ngong kuwasawiri waandamanaji wa ODM kama wanaoneza fujo,” akasema Bw Sonko akihutubu eneobunge la Dagoretti Kusini mnamo Januari 24, 2021.