Habari za Kitaifa

Waislamu watofautiana vikali kuhusu kuanza kwa Ramadhan

Na CECIL ODONGO February 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TOFAUTI kali zimezuka kati ya Waislamu kuhusu lini wanastahili kuanza kufunga kwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan baada ya baadhi ya viongozi kupinga tangazo la Afisi ya Kadhi Mkuu kuwa waanze kuangalia mwandamo wa mwezi Jumanne, Februari 17.

Viongozi hao wanasema kuwa kwa mujibu wa Sunnah ya Mtume Mohamed (SAW), mwezi unastahili kuangaliwa tarehe 29 ya mwezi wa Shaban (mwezi wa nane kwenye kalenda ya Waislamu) ambayo ni Jumatano Februari 18.

“Waislamu wote kote nchini wanaombwa waangalie mwezi (hilal) jioni ya Jumanne kisha wawasilishe taarifa iliyothibitishwa kwa Afisi ya Kaimu Kadhi Mkuu kupitia 0794339467,” ikasema notisi iliyotolewa mnamo Alhamsi Februari 12 kutoka kwa afisi ya Kadhi Mkuu.

Hii ina maana kuwa iwapo mwezi utaandama Jumanne, basi mfungo utaanza Jumatano Februari 18.

Iwapo mwezi hautaonekana, Ramadhan itaanza Februari 19 japo tangazo rasmi linatarajiwa kutoka kwa Afisi ya Kadhi Mkuu.

Mwenyekiti wa Baraza la Maimamu na Wahubiri (CIPK) ukanda wa Kaskazini mwa Bonde la Ufa Sheikh Abubakar Bini alisema makadhi wakuu waliopita walikuwa wamekubali mwezi uangaliwe kieneo kwa ajili ya umoja wa Waislamu.

Hii pia inastahili wakati wa siku 29/30 ambazo mfungo wa Ramadhan unatarajiwa kukamilika.

Hata hivyo, kupitia maelewano hayo, Waislamu watafuata mwandamo wa mwezi wa Saudi Arabia baada ya kukamilika kwa Hajj ambayo ni sikukuu ya Eid Ul-Adha (sikukuu ya kuchinja) ambayo ni Juni 5 au 6 mwaka huu kutegemea siku mwezi utaonekana.

“Kadhi Mkuu anastahili kukoma kuwapotosha Waislamu kwa kusema tuanze kuangalia mwezi Jumanne ambayo ni siku 28 ya Shaban. Hakuna mwezi siku hiyo na hafuati dini, kwa hivyo tutakuwa tukiangalia mwezi upi? Mbona anaenda kinyume na makadhi waliohudumu hapo awali?” akauliza Sheikh Bini.

“Waislamu wampuuze na waanze kuangalia mwezi Jumatano ili tuanze kufunga Alhamisi,” akaongeza.

Baraza la Waislamu Kenya Fatwa pia limepinga notisi kutoka afisi ya kadhi mkuu, likisema mwezi unastahili kuanza kuangaliwa Jumatano na si Jumanne.

“Sote tuangalie mwezi kuanzia jioni ya Jumatano ambayo ni tarahe 29 ya Shaban 1447,” ikasema taarifa ya baraza hilo.

“Yeyote akiuona mwezi basi ambie baraza au kupitia maimamu au viongozi wa kidini wanaotambulika,” ikaongeza taarifa hiyo.

Tofauti hizo zinaashiria kuwa huenda Waislamu kutoka kaskazini mwa Kenya na wale wa Pwani pamoja na maeneo mengine wakaanza kufunga nyakati tofauti.

Waislamu kutoka kaskazini mwa Kenya wamekuwa na ada ya kufuata mwandamo wa mwezi unavyotangazwa na Saudi Arabia.

Nao Waislamu kutoka maeneo mengine ya Kenya na Pwani wamekuwa wakiwafuata mufti kutoka Tanzania na Zanzibar na wataalamu wengine wa kuangalia mwezi kutoka Afrika Mashariki.