Habari za Kitaifa

Wakazi wa Nairobi wanaoishi karibu na mito wapinga mpango wa kuwahamisha

Na LABAAN SHABAAN April 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAELFU ya wakazi wa Nairobi wanaoishi karibu na Mto Nairobi na katika maeneo yaliyo mkabala na mito midogo inayotiririsha maji katika mto huo wako kwenye hatari ya kupoteza mali ya thamani ya mamilioni ya pesa.

Hii ni kufuatia tangazo la serikali kufanya kingo za mto kuwa maeneo maalum ya mipango ya ustawishaji mazingira na biashara.

Issa Hassan ambaye ni mkazi aliyejenga makazi yake mita 10 kutoka mtoni Kawangware anapinga mpango huu.

“Sitaki pesa yoyote ya fidia kwa sababu ya ardhi yangu. Wakinitoa hapa wanipeleke Ruai ama Mombasa wataniharibia maisha yangu na ya watoto wangu,” akasema Bw Hassan.

Mkazi mwingine ni Faith Minayo ambaye anaambia Taifa Leo kuwa ni mzaliwa wa eneo la Riruta Muslim Village karibu na mto.

“Mimi siko tayari kuhama na endapo nitaondoka eneo hili serikali haiwezi kunilipa hata nikiwa na hatimiliki ya ardhi,” akasema Bi Minayo.

Ukanda wa mita 60 umetengwa kutoka mtoni kuwa eneo la chemchemi katika mita 30 na sehemu iliyobaki kustawishwa kwa miradi ya serikali.

Maeneo yatakayoathiriwa ni kutoka Naivasha Road hadi Ruai, kipaumbele kikiwa ujenzi wa nyumba za bei nafuu zinazoendelezwa na serikali ya Kenya Kwanza.

Mipango hii ni kulingana na notisi ya Machi 6, 2025 iliyotolewa na Waziri wa Mazingira Kaunti ya Nairobi Patrick Mbogo kutaka wananchi watoe maoni yao kwa kipindi cha majuma mawili kabla ya kutekelezwa kwa miradi.

Mkutano uliosimamiwa na washikadau wa serikali Kawangware kukusanya maoni ya wananchi ulivurugika juma lililopita kwa sababu ya kukosekana kwa mwafaka.

Wakazi waliozungumza na Taifa Leo walionyesha mafadhaiko yao kuhusu miradi ya serikali.

“Makaburi ya babu zetu yako hapa na hatufai kuenda mbali nayo. Naomba serikali iangalie tena mpango huu na kusikiza malalamishi yetu,” akasema Ali Macharia mwenye umri wa miaka 74.

Naye mkazi mwenzake Issa Macharia akaongeza: “Sisi hatutasonga hata inchi moja na hawafai kukaribia mashamba yetu na kukiuka haki zetu.”

Serikali ya Kaunti ya Nairobi inasema hatua hii imechochewa na ombi kutoka kwa Wizara ya Ardhi, Ujenzi, Makazi na Ustawishaji.

Serikali kuu inaendesha mpango wa ujenzi wa nyumba za bei nafuu katika kingo za Nairobi River pamoja na uboreshaji wa mazingira ya mito kudhibiti wa mafuriko.