Habari za Kitaifa

Wakazi wadai Raila alitoa ardhi isiyo yake kwa mradi wa nyumba

Na DOMNIC OMBOK June 5th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

HALI ya taharuki inazidi kutanda katika Kaunti ya Kisumu huku wakazi wa maeneo ya Korando na Kogony wakitishia kuzuia ujenzi wa nyumba unaogharimu Sh128 bilioni katika ardhi ambayo kiongozi wa ODM Raila Odinga alitoa kwa mradi huo.

Wakazi hao wanawashutumu maafisa wa serikali kwa kunyakua ardhi ya mababu zao bila kushauriana na jamii.

Mradi huo unaosimamiwa na GulfCap Real Estate umezua utata zaidi kufuatia tangazo lililotolewa na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kuwa atatoa ekari tano kusaidia ujenzi wa nyumba za bei nafuu.

Shamba linalozozaniwa ni la ekari 285 ambalo zamani lilikuwa Kiwanda cha Kisumu Molasses na sasa imetengwa kwa ujenzi wa mradi mkubwa wa makazi unaoitwa LV Marina.

Ijapokuwa Bw Odinga ametetea mchango huo kama muhimu kukidhi mahitaji ya makazi eneo hilo, hatua hiyo imezua ghadhabu miongoni mwa wakazi wanaoiona kama isiyo ya kawaida na kinyume cha sheria.

Wiki jana, Bw Odinga alitangaza kuwa ametoa ekari tano za ardhi kwa mradi huo wakati wa ziara ya Rais William Ruto.

“Alichofanya Waziri Mkuu wa zamani kilikuwa kinyume cha sheria. Tunataka ardhi yetu irudishwe kama ilivyochukuliwa kutoka kwa mababu wetu mwaka wa 1979 kwa ajili ya kiwanda. Mradi huo ulipofeli, ilipaswa kurudishwa kwetu,” alisema George Weda, Katibu Mkuu wa Chama cha Ustawi wa Kisumu.

Kulingana na wazee wa jamii na hati zilizotajwa na chama, ardhi hiyo ilichukuliwa mwaka wa 1976 na aliyekuwa Waziri wa Masuala ya Kigeni wakati huo Dkt Robert Ouko chini ya Sheria ya Dhamana ya Ardhi (Sura ya 288). Ilipaswa kuwekwa amana kwa manufaa ya watu wa Kogony na Korando.

Kiwanda cha Kisumu Molasses, kilichozinduliwa mwaka wa 1977, kilidhaniwa kingetoa nafasi za kazi na miundo msingi katika eneo hili. Hata hivyo, wakazi wanasema ahadi hizo hazikutimia na kituo kilikwama katika miaka ya 1980.

Mzozo uliongezeka katika miaka ya 1990 wakati familia ya Odinga, kupitia Hazina ya Maendeleo ya Kisumu iliripotiwa kununua mali ya kiwanda hicho katika mnada wa hadhara. Hata hivyo wakazi wanahoji kuwa mnada huo ulijumuisha mashine pekee na sio ardhi.

“Mitambo pekee ndizo zilipigwa mnada. Ardhi ilibaki ya jamii,” Weda alishikilia.

“Tunahitaji kuelewa jinsi maendeleo haya yataathiri maisha yetu. Ni ardhi yetu na tuna haki ya kuhusishwa,” barua hiyo ilisema.

Kikundi kimetoa madai manne muhimu ikiwa ni pamoja na Tathmini ya kina ya Athari kwa Mazingira, ushirikishaji wa jamii, fidia ya haki kwa wakulima walioathiriwa na ukaguzi wa uwazi wa umiliki wa ardhi.

Wanasema kuwa eneo la mradi ni muhimu kwa ikolojia na muhimu kwa afya ya Ziwa Victoria.