Wakenya mitandaoni wamshambulia Ruto kwa kumpongeza Museveni
WAKENYA watumiaji mitandao wamekita kambi katika chapisho la Rais William Ruto la kumsifia Rais Yoweri Museveni, 81, kwa ushindi wake katika uchaguzi wa Januari 15.
Watumiaji mitandao walieleza kushangazwa na pongezi hizo wakisema kulikuwa na kila dalili kwamba uchaguzi mkuu wa Uganda haukuwa huru wala wenye haki na kwamba uligubikwa na dhuluma na vitisho dhidi ya mpinzani wake mkuu, kiongozi mchanga Bobi Wine, 43.
“Baada ya kutangazwa rasmi kwamba umechaguliwa tena kwa muhula mwingine, nakupa pongeza kwa niaba ya serikali na niaba ya Wakenya,” ikasema barua aliyoweka kwenye chapisho lake kwenye X.
SOMA Chapisho la Ruto likipongeza ushindi wa Museveni
Wengi haswa walikejeli aya ya pili ya barua hiyo iliyosema kwamba ushindi wa Bw Museveni ulikuwa usiopingika na kwamba ulikuwa idhibati ya mapenzi ya dhati ya raia wa Uganda kwa chama chake NRM.
“Unawezaje kupongeza Museveni baada ya uchaguzi ambao intaneti ilizimwa, jeshi kumwagwa barabarani, viongozi wa upinzani kukamatwa na wananchi wa kawaida kupigwa kwa kuhudhuria mikutano ya kampeni za Upinzani,” mtumiaji mtandao kwa jina Political Analyst akauliza.
Mwingine, kwa jina Jefahh, akaandika: “Waafrika wenzetu, sisi kama Wakenya hatukubaliani na kile alichosema Rais Ruto. Mtazamo wake ni wa kibinafsi na hausimamii kile mamilioni ya Wakenya wanafikiria. Tunasimama na raia wa Uganda kusema kwamba hakukuwa na uchaguzi.”
“Ndugu mpendwa, nchi zetu mbili zinaunganishwa na ushirikiano wa kihistoria ambao utanufaika na kujitolea kwako,” ikaendelea kusema barua ya Rais Ruto huku akiahidi ushirikiano kutoka kwa serikali yake.
Hata hivyo, Rais alipata waliohisi hatua yake ilikuwa sahihi.
“Ahsante Rais, tunashukuru na tuna furaha kuhusu ushirikiano wa nchi zetu; hongera sana,” Gerald Mubangizi akamjibu Ruto.
Kunao walioona kwamba Dkt Ruto kama kinara wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hakuwa na budi ila kutambua ushindi wa Museveni, Uganda kama mwanachama wa EAC.
Marais wengine wa EAC akiwemo Rais Paul Kagame wa Rwanda alituma pongezi zake Jumatatu, Januari 19, 2026 na mufa mfupi baadaye, Rais wa Tanzania Samia Suluhu pia akatundika ujumbe wake wa heri njema kwa mkongwe Museveni.