Habari za Kitaifa

Wakurugenzi wa Nairobi Hospital washtakiwa kukiuka sheria za kampuni

March 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAKURUGENZI wanne wa Bodi ya Hospitali ya Nairobi wanaokabiliwa na changamoto kali za kutimuliwa walishtakiwa Jumatatu, Machi 16, 2026 kwa kujipatia zaidi ya Sh8 milioni na kutomkabidhi msajili wa kampuni katika afisi ya mwanasheria mkuu taarifa za kifedha.

Dkt Job Lukuru Obwaka, 80, Dkt Chris Bichage, Wakili Samson Mbuthia Kinyanjui na Dkt Valerie Akinyi Gaya walishtakiwa baada ya kuzuiliwa korokoroni wikendi.

Madaktari hao wenye tajriba ya juu katika masuala ya tiba waliomba mahakama kupitia kwa mawakili wao waachiliwe kwa dhamana huku wakisema “hawawezi kutoroka kutokana na huduma wanazotoa kwa Wakenya.”

Washtakiwa hao wanne walifikishwa kortini baada ya kupinga kwa zaidi ya mwaka mmoja hatua ya Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Jinai (DCI) kuwachunguza.

Wakurugenzi wa Nairobi Hospitali Job Lukuru Okwaka na Chris Bichage Munga Nyamaratandi mahakamani Machi 16, 2026. Picha|Richard Munguti

Mahahakama ilielezwa pia na wakili Rodgers Sagana kwamba madaktari hao walishtakiwa kutowasilisha kwa msajili wa kampuni katika afisi ya mwanasheria mkuu taarifa za mapato ya Nairobi Hospital kinyume cha sheria.

Dkt Bichage alishtakiwa kwa kujifaidi na Sh4.8m kutoka kwa kampuni ya bima ya Meritorious Insurance Agency iliyokuwa imepewa kandarasi ya kutoa huduma kwa Nairobi Hospital.

Shtaka lilisema Dkt Bichage, alipokea pesa hizo kutokana na wadhifa wake wa ukurugenzi.

Naye Bw Kinyanjui alikana kupokea Sh3,999,995 kutoka kwa kampuni ya bima ya Meritorious kinyume cha sheria.

Mahakama ilielezwa na mawakili wanaowatetea washtakiwa kwamba adhabu ya makosa wanayodaiwa kufanya ni faini ya Sh200,000.

Hakimu aliwaachilia washtakiwa kwa dhamana ya Sh5 milioni.

Kesi itatajwa Machi 31, 2026 kwa maagizo zaidi.