Walimu wasimulia Waziri Duale mateso makuu wanayopitia mikononi mwa SHA
WAZIRI wa Afya Aden Duale jana alifanya kikao akilenga kuzuia mzozo uliokuwa ukitokota kati ya Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) na walimu waliotishia kujiondoa kwenye mpango huo wakilalamikia huduma duni.
Bw Duale aliitisha kikao kilichowaleta pamoja viongozi wa SHA, maafisa wa vyama vya walimu (Kuppet na Knut) na Tume ya Huduma ya Walimu (TSC).
Hatua hiyo ilifuatia notisi ya siku saba iliyotolewa na KUPPET wiki iliyopita, ikitaka matatizo yanayokumba mpango wa bima ya afya ya walimu yashughulikiwe haraka.
Zaidi ya walimu 400,000 kwa sasa wananufaika na bima ya afya chini ya mpango huo.
Katibu Mkuu wa KUPPET, Bw Akello Misori, alisema walimu wanataka ufafanuzi kuhusu manufaa wanayostahili na pia matatizo ya mfumo wa kidijitali unaotumiwa na hospitali.
“Tulitaka ufafanuzi kuhusu manufaa ya walimu na pia changamoto ya mfumo ambao hospitali zinasema ni wa polepole, hali inayowatatiza walimu. Pia kuna tatizo la viwango vingi vya idhini kabla ya mwalimu kutibiwa,” alisema Bw Misori.
Hata hivyo, kulingana na baadhi ya watu waliohudhuria mkutano huo, Waziri hakuzungumzia kikamilifu mapengo makubwa ya ufadhili na changamoto nyingine muhimu ndani ya mpango wa SHA.
Malipo ya baadhi ya gharama za matibabu ambayo hayajalipwa tangu Desemba 2025, pia hayakushughulikiwa ipasavyo. Kampuni za bima zinasema haziwezi kugharamia gharama hizo, hali inayolazimu TSC kubeba mzigo huo. Hata hivyo, TSC imesema haina fedha za kutosha na imeomba ufadhili wa ziada.
Maafisa wa KUPPET pia walitaka walimu zaidi ya 20,000 walioajiriwa vibarua wajumuishwe katika mpango wa bima ya afya. TSC ilisema itahitaji takriban Sh1 bilioni ili kuwajumuisha walimu hao.
Kuhusu matibabu nje ya nchi, walimu wanaweza kupata huduma katika hospitali tisa zilizoidhinishwa, tatu nchini Uturuki, nne India na mbili Saudi Arabia.
Hospitali 11 pia zimeidhinishwa kutoa huduma za matibabu ya uzazi kwa njia ya IVF.
Kwa muda sasa walimu wamekuwa wakilalamika kuwa baadhi ya hospitali hukataa au huchelewa kuwahudumia zikisisitiza walipe pesa taslimu.
Malalamishi hayo yaliongezeka mwezi uliopita baada ya baadhi ya walimu waliohusika katika ajali ya barabarani kudaiwa kunyimwa matibabu katika hospitali kadhaa licha ya kuwa katika hali mbaya.
Alipozungumza na wanahabari katika Afya House baada ya mkutano huo, Bw Duale alionya hospitali zilizoidhinishwa na SHA dhidi ya kuwanyima wagonjwa huduma.
“Ikiwa tutagundua kuwa mnakataa kuwahudumia Wakenya na kuwanyima haki yao ya kikatiba ya kupata huduma za afya, tutawasimamisha kutoka kwenye mfumo wa SHA na hata kufuta leseni zenu za kufanya kazi,” alionya.
Alisema ni jambo lisilo la kibinadamu kwa baadhi ya hospitali kuweka fedha mbele kuliko maisha ya watu kwa kutoa visingizio kuwa SHA haijazilipa.
Bw Duale alisema hospitali zote na mkataba na SHA zinapaswa kufahamu kuwa malipo yao yanafanywa kulingana na sheria, ambayo inaeleza kuwa malipo yanapaswa kufanywa ndani ya siku 90.
Mnamo Jumatatu usiku, SHA ilitoa Sh4.1 bilioni kwa vituo vya afya vya huduma ya msingi kote nchini kulipia huduma zilizotolewa kati ya Oktoba na Januari.
Aidha, kiasi kingine cha Sh11.3 bilioni kinatarajiwa kutolewa kufikia Machi 14, 2026 kwa hospitali za umma, binafsi na zile za mashirika ya kidini.