Wasiwasi Kenya ikikumbwa na uhaba wa virutubishi vinavyozuia upofu kwa watoto
KWA miezi miwili sasa, Kenya imekumbwa na uhaba wa virutubisho vya Vitamini A kwa watoto, hali inayowaacha akina mama katika suitafahamu huku watoto wakiendelea kuwa katika hatari ya magonjwa yanayoweza kuzuiliwa.
Mnamo Jumanne asubuhi, Atieno Valentine aliwasili katika kituo cha afya eneo la Eastlands jijini Nairobi akiwa na binti yake wa miezi sita aliyestahili kupata dozi yake ya kawaida ya Vitamini A na chanjo ya mafua. Alipata chanjo pekee.
Aliambiwa kuwa Vitamini A imekuwa haipatikani kwa miezi miwili.
“Muuguzi aliniambia, ‘Leo tutampa chanjo ya mafua tu. Virutubisho labda mwezi ujao.’ Katika kliniki hiyo kulikuwa na kina mama waliokosa mwezi uliopita wakitarajia kupata mwezi huu. Lakini bado haikuwa,” alisema.
Virutubisho vya Vitamini A hutolewa bure mara mbili kwa mwaka kwa watoto wenye umri wa miezi sita hadi 59.
Ulimwenguni, vinatambuliwa kama mojawapo ya hatua za gharama nafuu zaidi za kuokoa maisha ya watoto.
Upungufu wa Vitamini A ni miongoni mwa visababishi vikuu vya upofu unaoweza kuzuiliwa kwa watoto na pia huchangia kwa kiasi kikubwa vifo vya watoto katika mazingira ya kipato cha chini.
Nchini Kenya, Wizara ya Afya inakadiria kuwa takriban asilimia 35 ya watoto walio chini ya miaka mitano wana viwango visivyotosha vya Vitamini A.
Tangu mwaka 1998, nchi imekuwa ikiendesha mpango wa kitaifa wa utoaji wa virutubisho vya Vitamini A mara mbili kwa mwaka, ukilenga watoto wote wa miezi sita hadi 59.
Hata hivyo, changamoto katika mfumo wa usambazaji zimekuwa zikisababisha mapengo ya mara kwa mara.
Dkt Walter Otieno, daktari wa watoto kutoka Magharibi mwa Kenya, alisema uhaba huo unaweza kuvumiliwa kwa muda mfupi lakini ni hatari iwapo utaendelea.
“Vitamini A si ya hiari. Hulinda macho, huimarisha kinga za mwili katika mapafu na utumbo, na ni muhimu sana kwa mfumo wa kinga. Watoto wasipopata, hasa wale ambao hawakunyonyeshwa au wenye utapiamlo, huwa katika hatari kubwa ya maambukizi,” alisema.