Habari za Kitaifa

Watatu wafa, wengine wengi kujeruhiwa baada ya jumba kuporomoka Kibera

Na DANIEL OGETTA April 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

JUMBA ambalo lilikuwa linabomolewa jana lilianguka mtaani Kibera na kusababisha vifo vya watu watatu huku wengine wengi wakisalia na majeruhiwa mbalimbali.

Mkuu wa Kupambana na Majanga Kaunti ya Nairobi Bramwel Simiyu alithibitisha mauti hayo na kusema watu wengine sita waliokolewa baada ya mkasa huo.

Jumba hilo lilikuwa limeanza kubomolewa Mtaa wa High-Rise Kibera.

Shughuli za kutafuta manusura zikiendelea katika eneo jengo liliporomoka Kibera, Aprili 8, 2026. Picha|Billy Ogada

Bw Simiyu alisema mafundi walivuruga msingi wa jumba hilo na kusababisha liporomoke.

Idadi ya watu ambao walikuwa wamekwama ndani haijabainika.

“Watu sita wamenusurika wakiwa hai na miili ya watu watatu imeondolewa.”

Watu wengine wako katika hali mbaya kiafya na wanaendelea kutibiwa hospitalini,” Bw Simiyu akaambia Taifa Leo.

Kulikuwa na hofu kwamba watu wengine bado walikuwa wamekwama ndani na juhudi za uokoaji bado zilikuwa zikiendelea.

“Idadi ya watu wasiojulikana bado wamekwama ndani. Makundi ya uokoaji yamefika na yanaendelea kuwaokoa raia,” ikasema chapisho la Red Cross kwenye mtandao wa X.