Watu 10 wafariki katika ajali ya barabarani Kariandusi
Watu wasiopungua kumi wamethibitishwa kufariki kufuatia ajali ya barabarani iliyohusisha trela na matatu ya kubeba abiria 14 katika eneo la Kariandusi karibu na Gilgil, kwenye barabara kuu ya Nairobi-Nakuru.
Ajali hiyo ilitokea Jumamosi asubuhi baada ya matatu iliyokuwa ikienda kasi kupoteza mwelekeo na kugonga trela iliyokuwa imesimama barabarani, na kuwaua watu kumi papo hapo huku wengine wakijeruhiwa.
Akithibitisha ajali hiyo, Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Gilgil, Winston Mwakio, alisema trela hiyo ilikuwa imeharibika na kusimama kando ya barabara kabla ya kugongwa na matatu hiyo.
Kulingana na kamanda huyo, athari ya mgongano huo ilikuwa kubwa na kusababisha vifo vya abiria 10 katika matatu hapo hapo.
Ripoti za walioshuhudia zinaonyesha kuwa watu wawili pekee walinusurika na walikimbizwa hospitalini kupokea matibabu.
Vikosi vya uokoaji, wakiwemo maafisa wa polisi na wakazi wa eneo hilo, walitoa miili kutoka kwenye mabaki ya gari kabla ya kufungua eneo la ajali.
Barabara hiyo ni mojawapo ya njia kuu zinazounganisha miji ya Nairobi na Nakuru, lakini imekuwa ikishuhudia ajali nyingi katika miaka ya karibuni.
Ajali hiyo inajiri siku chache baada ya Mamlaka ya Kitaifa ya Usalama Barabarani (NTSA) kutoa tahadhari kwa madereva dhidi ya uendeshaji wa kiholela hasa katika kipindi hiki cha sikukuu ya Pasaka.
Mkurugenzi Mkuu wa NTSA, Nashon Kondiwa, alitangaza kuwa mamlaka hiyo itaanzisha msako mkali dhidi ya madereva wanaokiuka sheria za barabarani na magari yasiyofaa barabarani ili kupunguza ajali.
Alisema NTSA itashirikiana na Huduma ya Polisi wa Kitaifa kuimarisha ukaguzi katika barabara kuu na mijini wakati huu wa shughuli nyingi za usafiri.