Habari za Kitaifa

Watu sita wafariki katika ajali ya helikopta Nandi

Na VITALIS KIMUTAI February 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAMBIRAMBI zinaendelea kumiminika kutokana na kifo cha Mbunge wa Emurua Dikirr Johana Ng’eno maarufu kama Ngong aliyeaga dunia Jumamosi kwenye ajali ya helikopta.

Bw Ng’eno amerejelewa kama kiongozi jasiri, mpenda watu, mtetezi wa haki na mwanasiasa ambaye alihakikisha haki na usawa kwa wote.

Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen alimrejelea Bw Ng’eno kama kiongozi aliyewaongoza watu wa eneobunge lake kwa ujasiri bila kuogopa kuweka wazi msimamo wake alipohisi mambo yanaenda mrama.

SOMA PIA: Hatua za mwisho za Mbunge Johana Ng’eno

“Alikuwa akishiriki miradi ya kuwainua wasiojiweza katika jamii hasa kwa wanamuziki na alifanya hivyo hadi mwisho,” akasema Bw Murkomen.

Kiongozi wa Wengi katika Seneti, Aaron Cheruiyot alisema mbunge huyo alikuwa mchapakazi ndiyo maana hata watu wa eneobunge lake walimuenzi.

“Alikuwa mtumishi wa watu ambaye alijituma sana kwa wakazi wa Emurua Dikirr. Atakumbukwa kwa miradi mingi hasa kukuza talanta mashinani,” akasema Bw Cheruiyot.

“Hizi habari zinasikitisha sana na itatuchukua muda kuhimili uchungu huu. Naombea familia changa ya Bw Ng’eno pamoja na walioaga katika ajali hiyo ya helikopta faraja na amani ya Mwenyezi Mungu,” akaongeza.

Mwenyekiti wa Tume ya Huduma za Mahakama (JSC) Isaac Ruto alimrejelea marehemu kama aliyesimama wima na kuwatetea watu wake.

Mbunge wa Emurua Dikirr Johana Ng’eno almaarufu Ngong aliyeaga dunia katika ajali ya helikopta Mosop, Kaunti ya Nandi, Februari 28, 2026. Picha|Hisani

“Wakati ambapo wengine waliingiwa na uoga, alisimama wima na ni kiongozi ambaye haikuwa rahisi kushawishiwa aachane na matakwa ya wanaeneobunge lake. Juhudi zake zilisaidia wasanii kuendeleza ndoto zao wakati wengi walikuwa wamewataliki,” akasema Bw Ruto.

Gavana Dkt Eric Mutai (Kericho) na mwenzake Susan Kihika wa Nakuru walisema kuwa jamii ya Kipsigis imepoteza pakubwa kwa kufiwa na msemaji wao.

“Hakuna maneno ambayo yanatosha kueleza mauti ya Ngéno. Alikuwa rafiki, ndugu na mwalimu wa kisiasa kwangu hasa kuhusu masuala ya siasa na utawala,” akasema Dkt Mutai.

“Aliniunga mkono wakati ambapo nilitorokwa na wanasiasa wengi hasa baada ya juhudi za kunitoa madarakani kugonga mwamba kwenye seneti. Ni mbunge pekee ambaye alihudhuria hafla ya kunikaribisha nyumbani baada ya tukio hilo,” akaongeza.

Gavana wa Bomet Hillary Barchok alisema kuwa Bw Ngéno atakumbukwa kama mtetezi wa wale ambao wamebaguliwa katika jamii na alikuwa akitoa maoni yake kuhusu dhuluma bila uoga.

Seneta wa Bomet Hillary Sigei alisema nchi imempoteza gwiji na mtumishi ambaye sifa zake za uongozi zitaenziwa na kizazi kijacho.

“Alikuwa na sera ambazo zililenga kuimarisha maisha ya raia na kubuni nafasi za ajira kwa Wakenya. Atakumbukwa na wenzake pamoja na wananchi kama mwanasiasa shupavu,” akasema Bw Sigei.

Wabunge Victor Koech (Chepalungu), Charity Kathambi (Njoro) na Richard Yegon (Bomet Mashariki) pia walimrejelea Bw Ngéno kama mtumishi wa raia ambaye alikuwa na sifa za uongozi za kupigiwa mfano.

UNAWEZA KUPENDA: Urafiki tata baina ya Ng’eno, Ruto na Rigathi