Habari za Kitaifa

Wezi waiba vikombe vitakatifu vya dhahabu katika kanisa la Pasta Ezekiel

Na KEVIN MUTAI June 6th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

SETI ya vikombe sita vilivyopakwa dhahabu, sanduku la agano, birika na ‘chuma takatifu ya meno saba’ ni miongoni mwa vitu vya thamani vilivyoibwa kutoka kwa Kanisa la Pastor Ezekiel Odero la New Life Church and Prayer Centre, katika tukio la uhalifu usiku lililotikisa wakazi wa Mavueni, Kaunti ya Kilifi.

Vikombe hivyo vinadaiwa kuwa viliagizwa kutoka Israeli na hutumika kwa ibada. Viliibwa mapema alfajiri ya Jumatatu.

Kanisa hilo, mojawapo ya maeneo ya ibada yanayojulikana zaidi katika eneo hilo, sasa limeingia kwenye orodha ya yanayolengwa na wimbi la uhalifu ambalo limewaacha wakazi wengi wakiwa na hofu kubwa.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti Joseph Ongaya alisema washukiwa watatu tayari wamekamatwa na uchunguzi unaendelea.

“Tayari tuna washukiwa watatu rumande kuhusiana na wizi huo na tunashirikiana kwa karibu na kampuni za kibinafsi za ulinzi kubaini mianya iliyowezesha tukio hili,” Ongaya aliambia Taifa Leo.

Maafisa kutoka Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) walifika kanisani kukusanya ushahidi.

Baada ya kumhoji mshukiwa mmoja, wanaamini huenda wizi huo ulipangwa kwa usaidizi wa mtu wa ndani.

“Tunashuku baadhi ya wafanyakazi wa kanisa. Kuna ushahidi kwamba kulikuwa na watu ndani ya kanisa wakati tukio hilo lilipotokea,” aliongeza Ongaya.

Mbali na vitu vilivyopakwa dhahabu na vya ibada kama sanduku la agano, vitu vingine vya thamani pia vinaripotiwa kuibwa kutoka madhabahuni na maeneo ya karibu.

Tukio hili limeongezea orodha ya wizi unaozidi kuongezeka katika Mavueni na vijiji jirani ambapo majambazi wanafanya mashambulizi usiku wakiwa na ujasiri mkubwa, na kuwalenga watu binafsi na taasisi za kidini.