Habari za Kitaifa

Wito sheria irekebishwe kuruhusu wajane kurithi mali ya waume zao hata wakiolewa tena

Na SAM KIPLAGAT February 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JAJI mmoja amewataka wabunge kurekebisha vifungu kadhaa kwenye Sheria ya Urithi alivyosema haviendelezi haki kwa wajane wanaoamua kuolewa tena.

Mahakama Kuu mnamo 2022 iliamua kuwa sehemu kadhaa za sheria ya sasa ya urithi zinadhibiti haki ya mjane kurithi mali ya mume endapo ataamua kuolewa na mume mwengine.

Hata hivyo, Jaji Reuben Nyakundi alisema wanawake wengi wakati huu bado wanaogopa kudai haki zao kutokana na tamaduni katika jamii nyingi zinazopendelea wanaume kuliko wanawake.

Jaji huyo alisema mjane anafaa kuwa huru kuolewa kwa mara nyingine bila kupoteza haki yake ya kurithi mali ya mumewe wa kwanza.

Alieleza kuwa chini ya sheria ya sasa, urithi wa mjane unaweza kutwaliwa au urudishwe kwa jamaa za marehemu mumewe endapo ataamua kuolewa tena na mume mwingine.

“Kwa mtazamo wangu, kuna haki sawa kwa mume na mke kuingia katika ndoa mpya baada ya ndoa ya kwanza kuvunjwa kutokana na kifo. Mabadiliko haya hayafai kutumia kumhini mjane haki yake ya kurithi mali ambayo ilipatikana wakati wa ndoa yake ya kwanza,” akaeleza Jaji Nyakundi.

Sehemu ya 35 (1)(b) na 36(1)(b) ya Sheria ya Urithi zilikuwa zimesema kwamba mjane angepoteza haki yake ya kurithi mali ya marehemu mumewe wa kwanza endapo ataamua kuolewa na mume mwengine.

Hata hivyo, mwanamume aliyefiwa na mke, hakukumbwa na vikwazo kama hivyo. Hii ndiyo maana mahakama iliamua kuwa sehemu hizo za sheria ya urithi zinakiuka katiba kwa sababu zinaendeleza ubaguzi kwa misingi ya jinsia.

Aidha, Mahakama Kuu iliamua kuwa sehemu hizo za sheria zinakiuka Kipengele cha 27 (4) cha Katiba inayoharamisha ubaguzi kwa misingi ya jinsia.

Hata hivyo, Jaji Nyakundi alisema kuwa majukumu ya wanawake katika familia za zamani ziliwafanya wanawake kutumia wanaume katika umiliki ya mali, hasa chini ya sheria ya kitamaduni.

Alisema kwa misingi hiyo wajane hutarajiwa kusalia chini ya usimamizi wa familia za wanaume zao, na wakiolewa tena watakuwa chini ya mashemeji yao wapya.

Mahakama hiyo pia ilisema kuwa siyo haki kwa familia nyingi kuendelea kuhakikisha kuwa mali inasimamiwa na wanaume pekee.

Kulingana na Jaji Nyakundi wabunge wanapoifanyia marekebisho sheria ya urithi sharti wazingatie suala hili kwa sababu linahusu haki za kibinadamu na hitaji la kikatiba kuhusu usawa.