Wito watahiniwa wajiandikishe KCSE ikibaki na miaka miwili pekee itokomee
WAKENYA wana mwaka huu na mwaka ujao pekee kufanya Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne (KCSE) chini ya mfumo wa 8-4-4 kabla ya taifa kukumbatia kikamilifu Mfumo wa Umilisi na Utendaji (CBE).
Afisa Mkuu Mtendaji wa Baraza la Kitaifa la Mtihani (KNEC) David Njengere ametoa wito kwa watahiniwa wote ambao wangependa kufanya KCSE wajisajili kabla ya makataa yaliyowekwa.
KCSE imekuwepo tangu 1985 ilipoanzishwa katika mfumo wa 8-4-4.
Kwa mujibu wa KNEC, wanafunzi wana mwaka huu na mwaka ujao pekee kufanya KCSE kabla ya mfumo wote wa elimu kuingia CBE.
Watahaniwa wa mwisho wa KCSE kwa sasa wapo katika Kidato cha Nne.
KNEC imeanzisha hamasisho kuwarai wanafunzi au wale ambao wangependa kurudia KCSE kuanza kujisajili mwaka huu.
“Hii ndiyo nafasi ya pili ya mwisho ya kufanya KCSE na wote ambao wanataka kufanya mtihani huo au hata kuurudia mtihani lazima wajisajili katika muda uliowekwa. Muda huo upo kwenye barua ambayo imetumwa kwa wakurugenzi wa elimu katika kaunti ndogo na wakuu wa shule,” akasema Dkt Njengere kwenye mahojiano na Taifa Leo.
Aliwarai wazazi wasemezane na usimamizi wa shule kuhakikisha wanafunzi wao wamesajiliwa kwa wakati.
Katika mfumo wa CBE wanafunzi watasoma kwa miaka mitatu kwenye Gredi ya 10, 11 na 12 ambapo watawekwa kwenye matapo yanayolingana na kozi ambazo wanalenga kuzisomea.
Hii inatawarahisishia njia ya kujiunga na vyuo vikuu au taasisi za masomo ya juu.
Wanafunzi walioanza CBE kwa sasa wako Gredi ya 10 na watajiunga na vyuo vikuu au taasisi za elimu ya juu 2029.
Tayari vyuo vikuu na taasisi za masomo zimeanza kuwapa wahadhiri mafunzo ili kuwaandaa kuwapokea wanafunzi hao.
KNEC ilifafanua kuwa wanafunzi wanaweza kujisajili kufanya masomo saba au zaidi au kwa baadhi ya masomo tu.
Wanaojisajili kwa masomo saba au zaidi watapata alama za wastani na cheti huku waliojisajili kwa baadhi ya masomo yasiyofikia saba wakipata nakala ya matokeo.
Hata hivyo, watahiniwa wanaorudia KCSE hawawezi kufanya masomo tofauti na yale waliyofanya mwaka walioufanya mtihani huo mara ya kwanza.
Ili kujisajili kurudia KCSE, watahiniwa lazima wajisajili katika afisi ya mkurugenzi wa elimu katika kaunti ndogo ambapo watajisajili kama watahiniwa wa kibinafsi.
Ada ya mtihani kwa wanaorudia KCSE ni Sh7,200 na italipwa moja kwa moja kwa KNEC kupitia eCitizen.
Usajili kwa watahiniwa wa KCSE 2026 ulianza mwezi uliopita na utafungwa mnamo Machi 31, 2026 na tayari baraza hilo limeonya kuwa muda huo hautaongezwa.