Hamtanitisha, Ruto aambia upinzani
RAIS William Ruto jana aliapa hatatishwa na maneno ya wapinzani wake, akisisitiza kuwa atazidi kuhimiza maendeleo na umoja wa kitaifa huku akikosoa vikali upinzani kuwa hauna maono na mpango.
Akizungumza katika maadhimisho ya kila mwaka ya Wakulima wa Maziwa wa Meru yaliyofanyika katika uwanja wa Meru Dairy Farmers Cooperative, Rais Ruto alisema serikali yake tayari imetekeleza sehemu ya ahadi zake katika sekta za kilimo, elimu, afya, na ajira.
Rais alikuwa ameandamana na Naibu wake Prof Kithure Kindiki, Waziri wa Ushirika Wycliffe Oparanya, Gavana wa Meru Isaac Mutuma, pamoja na wabunge kadhaa wa eneo hilo.
Matamshi ya Rais yalijiri huku aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua akiendelea na ziara yake ya pili kaunti ya Meru, ambapo alimkashifu Rais kwa kutotimiza ahadi za Kenya Kwanza.
“Nimekuwa kwenye siasa kwa muda mrefu sana kiasi kwamba siwezi kutishwa na kelele za kisiasa. Sina muda wa kupoteza na propaganda. Wanaopinga serikali hawana mpango wowote wa kuendeleza nchi,” alisema Rais Ruto.
Rais aliwataka wakazi wa Meru, waliompigia kura kwa wingi mwaka wa 2022, kuendelea kuunga mkono serikali akisema “ni serikali yao na inapaswa kuwahudumia.”
Katika mkutano huo, Rais alitangaza hatua kadhaa za kusaidia wakulima wa maziwa, ikiwemo kupunguza bei ya mbegu bora za ng’ombe kutoka Sh5,000 hadi Sh1,000 kuanzia Julai 1 mwaka huu.
Aliahidi pia kuwa serikali itatoa Sh100 milioni zaidi kuendeleza ujenzi wa kiwanda cha kutengeneza chakula cha mifugo, mradi wa thamani ya Sh400 milioni.
“Chakula cha mifugo kinachangia hadi asilimia 60 ya gharama ya uzalishaji wa maziwa. Ndiyo maana serikali yangu inashirikiana na Meru Dairy kuhakikisha bei ya chakula inapunguzwa ili wakulima wapate faida zaidi,” alisema.
Rais alieleza kuwa serikali itaondoa ushuru kwa wauzaji wa chakula cha mifugo wanaoagiza mahindi ya njano (kutoka nje, kama njia ya kupunguza gharama ya uzalishaji.
Katika juhudi za kukabiliana na maradhi ya mifugo, Rais Ruto alitangaza kuwa serikali itazindua kampeni ya kitaifa ya chanjo wiki ijayo.