Habari

Hasara moto ukiteketeza vibanda katika ‘Marikiti’ ya Kisii

Na WYCLIFFE NYABERI June 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAMIA ya wafanyabiashara wanaouza mazao mabichi na nafaka katika soko la Manispaa ya Kisii wanahesabu hasara baada ya moto kuteketeza vibanda vyao Jumapili asubuhi.

Moto huo, wenyeji na wafanyabiashara walisema, ulianza baada ya saa sita usiku wakati wengi wao walikuwa kwenye usingizi na hivyo basi hawakuwa na uwezo wa kuokoa chochote.

Bosire Ondieki, mmoja wa wafanyabiashara walioathirika alisema alipata hasara ya zaidi ya Sh500,000.

Yeye ni muuzaji wa karoti na mboga zingine.

Bosire alidokeza kuwa alikuwa amepokea shehena kubwa ya bidhaa anazouza Jumamosi jioni lakini hakuwa amewalipa wasambazaji wake.

“Nimemalizwa kabisa. Matumaini yangu yote yalikuwa hapa lakini sasa yamewaka moto ndani ya sekunde chache. Kwa zaidi ya miaka 10 nimekuwa katika soko hili, sijawahi kushuhudia hasara kama hii iliyosababishwa na moto,” Bw Bosire alilalamika.

Wafanyabiashara wakikadiria hasara katika Soko la ‘Marikiti’ ya Kisii. Picha|Wycliffe Nyaberi

Kakake mkubwa, Mokaya Ondieki pia ni mwathirika mwingine. Alisema pia amepoteza bidhaa zenye thamani ya Sh400,000.

“Soko hili limekuwa tegemeo langu pekee la mapato. Ni kupitia soko hili ambapo nimesomesha wanangu. Nimekuwa nikiuza kila aina ya mazao ya shambani kwa zaidi ya miaka 15 hapa na mke wangu lakini nimeamka asubuhi moja na kukuta hatuna chochote,” Mokaya alisema.

Kando yake, Alex Obiri, 26, alijishika tama akitazama kwa uchungu vibanda vilivyoungua.

Yeye, tofauti na wafanyabiashara wengine, alikuwa akilia kilio tofauti. Ingawa hakuwa mfanyabiashara, alikuwa akiishi kwa kuuza mifuko ya kubebea mizigo kwa mamia ya wanunuzi wanaojaa marikiti hiyo wakati wa wikendi.

“Soko hili huwa na shughuli nyingi na ninaitegemea tu kuendesha maisha yangu. Napata angalau Sh400 kwa siku kwa kuuza tu mifuko ya kubebea mizigo lakini sasa sijui nitapata wapi pesa hizo,” Obiri alisema.

Kufuatia moto huo, baadhi ya wafanyabiashara waliofika sokoni asubuhi wakiwa na bidhaa zingine walianza kuuzia katika barabara inayoekea katika Hospitali ya mafunzo na Rufaa ya Kisii, KTRH.

Chanzo cha moto huo bado hakijabainika lakini Kamanda wa Polisi Kaunti ya Kisii Ronald Kirui alisema uchunguzi kuhusu kisa hicho umeanza.

“Tunawahurumia wafanyabiashara ambao wamepoteza mali ya mamilioni ya pesa. Tumeanzisha uchunguzi wetu kujua kilichosababisha moto huo,” bosi huyo alisema.

Kumekuwa na mzozo kuhusu umiliki wa kipande cha ardhi ambacho wafanyabiashara hao wamekuwa wakifanyia biashara zao tangu zamani.

Lakini uamuzi wa hivi majuzi wa mahakama ya Kisii, ulitambua kuwa kipande hicho cha ardhi ni mali ya aliyekuwa Waziri wa Elimu Profesa Sam Ongeri.

Picha ya mtazamo wa juu wa soko la Marikiti ya Kisii lililoungua usiku wa kuamkia Jumapili. Ardhi ya soko hilo imo kwenye mzozo baina ya EACC na familia ya Profesa Sam Ongeri. Picha|Wycliffe Nyaberi

Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) ilikuwa ikitaka kukitwaa kipande hicho cha ardhi kilichoko mjini Kisii kutoka kwa mbunge huyo wa zamani wa Nyaribari Masaba, ikisema kuwa mkongwe huyo hakukipata kwa njia zinazofaa.

Lakini Jaji Sila Munyao wa Mahakama ya Kisii alikataa ombi la EACC kutangaza mali hiyo ya mamilioni kama ardhi ya umma, akisema kuwa kuwepo tu kwa wachuuzi wa mboga hakumaanishi kwamba mali hiyo ilikuwa ya umma.

Tume ya EACC iliwasilisha kesi hiyo mwaka 2010, ikidai kwamba ardhi hiyo ilichukuliwa kwa njia isiyo ya kawaida na kwa ulaghai na Profesa Ongeri kwani ilikuwa imetengwa kwa ajili ya Soko la Manispaa ya Kisii kupitia Mpango wa Maendeleo wa 1971.

Profesa Ongeri aliwahi kuwa waziri chini ya marais wendazao Daniel Moi na Mwai Kibaki. Kando na kuwa mbunge wa Nyaribari Masaba, pia aliwahi kuwa seneta wa Kisii na balozi.

Baada ya kufeli katika jaribio lake la kutaka awe gavana wa Kisii katika uchaguzi mkuu uliopita, Profesa Ongeri alitokomea kwenye ulingo wa kisiasa na kugeukia kilimo.