Habari

Hizi Sh2,000 tunazopokea hazitoshi chochote, wakongwe walilia serikali

Na NDUBI MOTURI March 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAKONGWE wamelalamika kuwa Sh2,000 za Inua Jamii wanazolipwa na serikali ni kidogo mno ikilinganishwa na hali halisi ya kupanda kwa gharama ya maisha.

Kwenye mahojiano na Taifa Leo, wakongwe kutoka maeneo mbalimbali walisema pesa hizo hazitoshi kukimu mahitaji yao.

Daniel Nyaundi kutoka Nyamira, ambaye anaugua saratani ya tezi dume alisema pesa hizo hazitoshi hata kugharimia safari zake za kuenda hospitalini kiasi kwamba anawategemea watoto wake wampe pesa za chakula.

Inua Jamii ilianzishwa na serikali mnamo 2013 ili kuwasaidia wakongwe ambao wamefikisha umri wa miaka 70 kupata Sh2,000 za kujikimu.

Ingawa idadi ya wanaonufaika imepanda, kiasi kinachosambazwa kimesalia kile kile Sh2,000.

David Owuor ambaye ni mwalimu mstaafu kutoka Koru, Kaunti ya Kisumu naye anasema kuwa bei ya bidhaa zimepanda na pesa hizo huisha tu baada ya kuzipokea.