Habari

Hofu baadhi ya masomo yakikosa wanafunzi Gredi 10

Na MERCY SIMIYU February 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BAADHI ya shule za upili za umma zimejipata katika hali ya sintofahamu baada ya kusajili wanafunzi wawili au watatu pekee katika masomo ya lugha na sanaa bunifu katika Shule ya Sekondari Pevu, hali inayoashiria visiki vya mapema katika utekelezaji wa mfumo wa Elimu Unaozingatia Umilisi (CBE).

Kwa mujibu wa vyanzo katika Wizara ya Elimu, mfumo wa awali ulipangwa kudumisha uwiano wa wanafunzi kutoka maeneo na asili mbalimbali.

Hata hivyo, mabadiliko ya hivi karibuni katika mchakato wa uteuzi yamevuruga uwiano huo, na kusababisha walimu kubaki na madarasa yenye idadi ndogo au mpangilio usio sawa wa wanafunzi.

Takwimu za Wizara ya Elimu zinaonyesha kuwa asilimia 51 ya wanafunzi wamejisajili katika masomo ya STEM, asilimia 38 katika sayansi za kijamii, huku asilimia 11 pekee wakichagua masomo ya sanaa na michezo.

Idadi hii ndogo imeibua maswali kuhusu uendelevu wa madarasa hayo, na utekelezaji bora wa mfumo wa CBE, huku masomo ya sayansi yakiendelea kuvutia wanafunzi wengi.

“Kwa kweli kuna shule ambazo hazina mwanafunzi hata mmoja katika mkondo fulani. Inategemea idadi ya wanafunzi waliopokelewa na ni wangapi wamechagua STEM, sayansi za kijamii au sanaa na michezo. Pia inategemea masomo ambayo wanafunzi wanayachagua kulingana na uwezo na maslahi yao,” alisema Dkt William Sugut, Mkuu wa Idara ya Elimu ya Sekondari Pevu.

Akizungumza na Taifa Leo Katibu wa Elimu ya Msingi Profesa Julius Bitok alisema wizara imetuma maafisa mashinani kutathmini hali hiyo, akisisitiza kuwa hatua zozote zitachukuliwa kwa kuzingatia mazingira ya kila shule.

Alisema maafisa hao wanachunguza mifumo ya usajili na kuangalia iwapo walimu wanaweza kuwaelekeza wanafunzi kwenye mikondo mbadala pale idadi inapokuwa ndogo kupita kiasi.