Homa Bay yasisimua kwa burudani Madaraka Dei ikimlaki Ruto kwa bashasha kuu
RAIS William Ruto na viongozi mashuhuri ambao walihudhuria sherehe za Madaraka Dei Jumapili walitekwa na burudani ya aina yake iliyowasilishwa na makundi mbalimbali katika uga wa Raila Odinga, Kaunti ya Homa Bay (ROSH).
Burudani hiyo ilijikita katika kuonyesha utamaduni wa jamii ya Waluo na ilisheheni kauli mbiu ‘Maji yetu, Thamani Yetu’ ikizingatiwa Homa Bay inapakana na Ziwa Victoria.
Katika burudani ya kwanza, zaidi ya wanafunzi 500 kutoka shule mbalimbali za kaunti hiyo waliimba nyimbo za kizalendo huku wakiunda michoro ya Homa Bay, Ziwa Victoria na samaki aina ya ngege.
Wanafunzi hao waliwasilisha mashairi kuhusu uchumi wa majini huku wakisakata pia tungo za wanamuziki mbalimbali ikiwemo wimbo wa benga wa mwanamuziki Dola Kabari.

Makundi ya wasakataji densi za kitamaduni yanayojumuisha Kagan, Kochia, Rachuonyo yakafuata huku wasanii wa Ohangla Aroji Chogo, Fredy Jakadongo, Kaka Talanta, Oluoch Digital, Papa T, Kevin Gombe na wasanii wa nyimbo za injili pia wakijumuika kwenye jukwaa.
Kwa wakati mmoja Rais, Kinara wa ODM Raila Odinga, Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki na Rais wa Slovenia Natasa Musar miongoni mwa wengine walioketi kwenye jukwaa kuu walisimama na kusakata densi huku wakifurahi nyimbo na midundo iliyoporomoshwa.
Tungo zilizowasilishwa zilikuwa za mchanganyiko wa Kiluo na Kiswahili na zilisifu Serikali Jumuishi na kutoa wito wa umoja nchini.
Kando na burudani, uwanja wa ROSH ulijaa hadi pomoni kufikia saa nne usiku wa kuamkia Madaraka Dei, huku waliokuwa uwanjani wakitumbuizwa hadi asubuhi.
Rais Ruto naye usiku huo alikutana na viongozi wa Homa Bay katika ikulu ndogo viungani mwa mji huo kuzungumzia utekelezaji wa miradi mbalimbali.
Kiongozi wa nchi alilakiwa kishujaa alipowasili ugani ROSH dakika chache baada ya saa nne asubuhi kwenye gari rasmi kisha akakagua gwaride la jeshi.
Aidha kulikuwa na maonyesho ya ndege za kivita kama tu sherehe nyingine za kitaifa na baada ya kumalizika kwa burudani, milango ya kuingia uwanjani ilifunguliwa na raia wakaingia na kuujaza uga huo.
Mnamo Jumatatu, Rais Ruto na Bw Odinga bado watakuwa Homa Bay ambako wanatarajiwa kuhudhuria debi ya Mashemeji kati ya Gor Mahia na AFC Leopards.