Hospitali za kaunti zamulikwa kwa ufisadi, wagonjwa wakilazimika kutoa hongo
TUME ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) imeorodhesha idara za afya za kaunti kama taasisi zinazokabiliwa na ufisadi kwa kiwango kikubwa zaidi ndani ya serikali za kaunti.
Hali ni mbaya kwani wagonjwa wanalazimika kutoa hongo kuhudumiwa na kupata dawa katika sekta iliyokusudiwa kulinda ustawi wa wananchi.
Utafiti wa EACC pia umefichua kuwa ofisi za uchukuzi na ardhi za kaunti ni sehemu zinazozongwa na ufisadi kwa kiwango kikubwa, ambapo wakazi mara nyingi hulazimika kutoa rushwa kabla ya kupata huduma muhimu.
Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti huo, rushwa nyingi hutolewa baada ya wahusika kutakiwa kutoa kitu, visa vikihusisha asilimia 43.3 ya matukio.
Zaidi ya asilimia 23.3 hulipwa na wananchi wanaotaka kupata huduma, huku asilimia 18 ikilipwa ili kuepuka kucheleweshewa huduma.
Huduma za afya ndizo zinazoathirika zaidi, zikihusisha asilimia 45.1 ya visa vya ufisadi vilivyoripotiwa.
Sekta ya uchukuzi ilifuata kwa mbali ikiwa na asilimia 9.1, huku kilimo kikiwa na asilimia 7.9 ya visa vya ufisadi.
Kamishna wa EACC, Dkt Cecilia Mutuku, alisema viwango hivi vimetokana na kutoridhika kwa wananchi na huduma zinazotolewa na serikali za kaunti.
Alibainisha kwamba wakazi wengi wanahisi kulazimika kutoa rushwa ili tu wapate huduma ambazo kwa kawaida zinapaswa kupatikana bila malipo.
“Katika sekta ya afya, kwa mfano, baadhi ya wagonjwa wanahisi lazima watoe rushwa ili kupata dawa kutoka hospitalini,” alisema Dkt Mutuku.
Alieleza kuwa matokeo haya yanatokana na utafiti unaofanywa kila mwaka na Tume, akiongeza kuwa sekta ya afya imekuwa tatizo kubwa mara kwa mara.
“Afya inaendelea kuibuka mara kwa mara. Miaka miwili iliyopita, tulifanya utafiti maalumu kuhusu sekta ya afya, na changamoto zinazokumba madaktari na wananchi zinahitaji hatua ya haraka,” alisema.
Maafisa wa tume hiyo ya kupambana na ufisadi walihimiza mabadiliko makubwa ndani ya sekta ya afya, wakionya kuwa baadhi ya watu bado wanaendelea kujipatia utajiri kwa gharama ya wananchi wa kawaida wanaotafuta huduma za matibabu.
“Lazima tuboreshe huduma za afya ili Wakenya wapate huduma bora bila kulazimishwa kutoa kitu chochote,” alisema Dkt Mutuku.
Dkt Mutuku alisema hayo aliposhuhudia uzinduzi wa Kamati ya Kaunti ya Kuzuia Ufisadi Homa Bay.
Kamati hizi, zinazoundwa na magavana, ni sehemu ya mkakati mpana wa Tume wa kubaini mapungufu ya mifumo na kuondoa maafisa wanaodai rushwa katika utawala wa kaunti.
Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha vita dhidi ya ufisadi kama msingi wa maendeleo endelevu.
“Lazima tujenge mifumo thabiti ya kuzuia ufisadi ikiwa tunataka kufanikisha maendeleo ya maana. Watu wengi wanahusisha EACC na utekelezaji, lakini kuzuia pia ni muhimu,” alisema.
Kupitia juhudi hizi, Tume imepata ushirikiano kutoka kwa Baraza la Magavana kusaidia kupunguza ufisadi katika serikali za kaunti.