Habari

Idara yachukua hatua kuwaepushia polisi mitego ya kimapenzi

Na KALUME KAZUNGU June 9th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

IDARA ya Polisi katika Kaunti ya Lamu, imechukua hatua kuepusha visa ambapo maafisa huhadaiwa na wanawake ambao huwashawishi kuwapa kiasi kikubwa cha fedha kabla ya kuwatenga.

Imebainika kuwa, baadhi ya wanawake huvizia maafisa wa polisi vijana wanaopelekwa katika operesheni za Lamu kwa mzunguko hadi kuwashawishi wengine wao kuchukua mikopo ya kuanzisha biashara.

Punde wanapogundua afisa amekaribia kukamilisha muda wake kwenye oparesheni, wanawake hao huanza kujitenga wakisubiri polisi wengine wageni.

Kamanda wa Polisi wa Lamu, Bw Kipsang Changach, amesema matumizi mabaya ya pesa ni miongoni mwa mambo ambayo yamekuwa yakiwasababishia polisi msongo wa mawazo.

Alisema wataalamu wa ushauri nasaha washatumwa kutoka Nairobi kuwapa polisi mawaidha.

Kulingana na Bw Changach, visa vingi vya polisi kujiua Lamu mara nyingi vimetokana na makadirio na matumizi mabaya ya hela zinazoacha maafisa wengi wakigubikwa na msongo wa mawazo.

Baadhi ya maafisa wa usalama waliozungumza na Taifa Leo, ikiwemo wale wa jeshi (KDF), polisi na magereza walikiri kujipata kwenye mtego na kuishia kukamuliwa hela nyingi.

“Najuta kutumia hela nyingi kwa kichuna niliyempata kwenye baa moja mjini Hindi. Alinidanganya, nikachukua mkopo na kufadhili biashara yake. Punde nilipotolewa Lamu binti alibadilisha nambari ya simu na kuhama alipoishi,” afisa aliungama.

Afisa mwingine alisema yeye binafsi pia alijikuta kwenye utata wa penzi la kiongo ila akajitambua mapema na kulikatiza mara moja.

“Hao akina dada wanatwaa mwanya wa kudanganya sisi polisi na jeshi, wakijua fika kuwa tunahudumu Lamu kwa muda. Punde tunapofanya operesheni na kipindi chetu cha kuondoka Lamu kinapojiri, wao hubadilisha namba na kutafuta walinda usalama wengine wanaokuja. Mimi nilijikwamua mapema la sivyo ningeambulia patupu,” akasema afisa mwingine.