Habari

Imamu ashtakiwa kulaghai muumini Sh774,000 kwa ahadi ya kumpeleka kuhiji Mecca

Na RICHARD MUNGUTI February 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

IMAM katika Msikiti ulioko mjini Malindi ameshtakiwa kwa kumlaghai muumini kitita cha Sh774,000 akidai atampeleka kuhiji jijini Mecca wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Omar Athman Omar alishtakiwa mbele ya hakimu mkuu mahakama ya Milimani Lucas Onyina.

Imam Omar alieleza mahakama kwamba mlalamishi katika kesi inayomkabili ni Mohamed Salim Bahlewa.

Kinara huyo wa msikiti alikana shtaka la kumlaghai Bahlewa kati ya Desemba 18 na 19, 2026.

Mahakama ilielezwa na Imam Omar kwamba aliondoka humu nchini Desemba 9, 2025 kwenda Saudi Arabia kushughulikia masuala ya dini.

Alimweleza hakimu kwamba akiwa Saudia mlalamishi alilipa pesa hizo za kufanikisha safari yake kuhiji Mecca.

Mshtakiwa aliambia mahakama kwamba alirejea nchini Feburuari 7, 2026 lakini “akatiwa nguvuni kama gaidi.”

Imam Omar aliambia hakimu, “Nilipofika uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta –JKIA- nilitoa pasipoti yangu kwa afisa wa idara ya uhamiaji ikaguliwe. Mara hiyo hiyo nilitiwa nguvuni nikapelekwa kituo cha polisi cha Kilimani na sikupata fursa ya kuwasiliana na mlalamishi,” alisema Imam Omar.

Aliomba aachiliwe kwa dhamana akisema “yeye ni kiongozi shupavu katika masuala ya dini ya Kiislamu na kwamba hawezi kushiriki katika mambo ya rushwa.”

Mhubiri huyo wa masuala ya dini alisukumwa rumande hadi Feburuari 10, 2026 hakimu atakapoamua ikiwa atamwachilia kwa dhamana au la.