Ipoa kuchunguza vifo vya watu watatu wanaodaiwa kuuawa na polisi
Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) imetuma timu ya maafisa kuchunguza mauaji ya watu watatu wanaodaiwa kupigwa risasi na polisi Alhamisi huko Transmara Kusini, Eneobunge la Kilgoris, Kaunti ya Narok.
Watatu hao walikuwa miongoni mwa kundi la raia waliovamia ardhi ya kibinafsi, ndani ya hifadhi ya Angama katika kijiji cha Loikuruk, wakidai kuwa shamba hilo lilinyakuliwa kutoka kwao na watu wenye ushawishi mkubwa nchini.
Katika hatua ya kijasiri, kundi hilo lilivamia ardhi hiyo ya ekari 800 kuanzia mwanzoni mwa wiki hii na kuitwaa.
Waliapa kusalia katika ardhi hiyo ambayo wanasema ni ya mababu na polisi wakatumwa kuwafurusha.
Hata hivyo, walipinga kufurushwa kwao na hilo likazua makabiliano makali kati yao na polisi.
Watu watatu walifariki dunia kutokana na majeraha ya risasi zilizodaiwa kufyatuliwa na maafisa wa polisi huku wengine kadhaa wakipata majeraha mbalimbali ambayo wanauguza nyumbani na hospitalini.
‘Mapema leo asubuhi, IPOA ilituma timu kuchunguza mauaji ya watu kadhaa na majeraha mabaya waliyopata wengine Alhamisi, Juni 5, 2025. Tukio hilo lilitokea baada ya polisi kudaiwa kufyatulia risasi kundi la watu walioripotiwa kuvamia ardhi ya kibinafsi,’ Mwenyekiti wa IPOA Ahmed Issack Hassan alisema katika taarifa.
Kisa hiki kinajiri zaidi ya mwezi mmoja baada ya watu wengine watano pia kuuawa kwa kupigwa risasi na maafisa wa polisi wa kitengo cha kukabili na fujo (GSU) katika eneo jirani la Angata Barrikoi, pia kutokana na mzozo wa ardhi.