Jacob Ocholla Mwai apambana kurithi mali ya Kibaki
ALIYEKUWA Mbunge wa Othaya Mary Wambui ni miongoni mwa watu 14 ambao huenda wakatoa ushahidi katika kesi ya urithi wa mali ya Rais wa zamani Mwai Kibaki.
Wakati huu Mahakama Kuu inaendesha uchunguzi kuhusu warithi halali wa mali yake na thamani halisi ya mali hiyo.
Stakabadhi mpya zilizowasilishwa mahakamani zinaonyesha kuwa mzozo unaozingira uhusiano kati ya Bi Wambui na Kibaki, hali ya mali yake na matibabu aliyopokea kabla ya kifo chake Aprili 2022 ni baadhi ya masuala yanayotarajiwa kuchipuza wakati wa kuzikizwa kwa kesi hiyo.
Familia ya Kibaki ikiongozwa na Judith Wanjiku Kibaki imeshtakiwa na watu wawili ambao ni Jacob Ocholla na Bi JNL, wote wanaodai ni watoto wa Kibaki. Wawili hao wanataka watambuliwe halali kama kama watoto wa Kibaki na hivyo wagawiwe mali yake.
Bw Ocholla na Bi JNL wamewasilisha ombi katika Mahakama Kuu, kitengo cha kutatua mizozo ya familia, wakitaka Bi Wambui agizwe kufika kutoa ushahidi kuhusu mali ya Kibaki.
Mawakili hao wanasema kuwa ushahidi atakaoutoa katika Mahakama hiyo, Nairobi na majibu atakaotoa akihojiwa na mawakili wa pande zote mbili, utakuwa muhimu katika kuhimili madai yao kwamba ni watoto halali wa Kibaki na hivyo wanapasa kugawiwa mali.
Hii ni licha ya kwamba majina yao hayako katia wosia ambao Kibaki aliacha. Kulingana na stakabadhi za mahakama. Mzozo wa muda mrefu kuhusu madai kuwa Bi Wambui alikuwa mkewe Kibaki, huenda ukafufuliwa.
Anatakiwa kutoa ushahidi au stakabadhi za kuonyesha kuwa aliolewa na Rais Kibaki chini ya sheria ya kitamaduni na haki yake katika mchakato wa urithi.
Wengine ambao wanatakiwa kuagizwa kutoa ushahidi kortini ni pamoja na Winnie Wangui Mwai na Maafisa Wakuu Watendaji wa Hospitali za Karen Hospitali, Nairobi Hospital na Shirika la Utafiti wa Kimatibabu cha Lancet.
Pia watakaohitajika kutoa ushahidi au stakabadhi ni Wakili Philip Coulson, Angela Wanjira Mbuthia, Anne Njeri Maina, David Wanjala na Otieno Clifford Richard.
Mawakili wa familia ya Kibaki Philip Murgor na Omoke Morara wanataka kuwahoji kuhusu rekodi za kisiri za kimatibabu kuhusiana na matibabu aliyopewa Kibaki hadi kifo cha mnamo Aprili 22, 2022.