Habari

Jiandae kukabili mafuriko, kaunti zaambiwa

Na NDUBI MOTURI March 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI imeagiza kila kaunti ndogo kuanzisha vituo vya taarifa kwa umma, vituo vya dharura na vituo vya kukabiliana haraka na mafuriko ili kuwasaidia wananchi wanaokumbwa na maafa.

Hii ni baada ya miundombinu muhimu kuharibiwa vibaya katika maeneo mbalimbali ya nchi kutokana na mito kufurika na maji kuharibu barabara na daraja.

Katika Makueni, Barabara ya Wote–Emali pamoja na daraja la Kyamelu zilifurika na kuathiri usafiri. Bungoma, daraja la watembea kwa miguu la Kimama lilisombwa na mafuriko.

Katika Migori, daraja kwenye mto Migori pia liliharibiwa vibaya baada ya kusombwa na maji ya mafuriko.

Jijini Nairobi, angalau shule 15 zimeathiriwa, huku madarasa na vifaa vya shule vikiharibiwa na maji ya mafuriko.

Rais William Ruto alisema mafuriko hayo yamesababisha mateso makubwa kwa familia nyingi nchini.

“Mafuriko yanayoendelea katika sehemu za Nairobi na maeneo mengine ya nchi yamesababisha vifo vya kusikitisha,” alisema Rais katika taarifa aliyochapisha kwenye mtandao wa X.

Mkuu wa Mawaziri, Musalia Mudavadi, alisema hali ya mafuriko katika Nairobi ni ya kutia wasiwasi na haikubaliki.